1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Adhabu ya kifo na kunyongwa yaongezeka duniani

Abdu Said Mtullya27 Machi 2014

Shirika la Amnesty International limetoa ripoti inayosema idadi ya watu waliopewa adhabu ya kifo na kunyongwa imeongezeka duniani. Ripoti hiyo inasema watu 778 walinyongwa mwaka jana katika nchi 22.

https://p.dw.com/p/1BWVj
Kamba inayotumika kunyingea waliohukumiwa adhabu hiyo
Kamba inayotumika kunyingea waliohukumiwa adhabu hiyoPicha: picture alliance/dpa

Je ni kosa gani linaloweza kusababisha mtu ahukumiwe adhabu ya kifo kati ya haya yafuatayo rushwa, uzinifu, biasharaya mihadarati, wizi wa gari au kutazama tamthilia iliyopigwa marufuku?

Jibu ni kwamba kila kosa kati ya hayo linaweza kusababisha mtu apewe adhabu ya kifo. Swali hilo limepelekwa katika mtandao wa internet na Shirika la kutetea haki za binadamu, Amnesty International ikiwa ni kiini cha ujumbe wa ripoti yake ya mwaka 2014 inayoitwa "Adhabu ya Kifo"

Ujumbe unasema adhabu ya juu kabisa ambayo mtu anaweza kuifikiria haitolewi kwa kosa la mauaji tu.

Kile ambacho katika nchi fulani kinazingatiwa kuwa ni kosa la mauaji kinategemea na utamaduni, dini na hali ya kisiasa ya nchi hiyo-Lakini pia hutegemea na jinsi wenye madaraka wanavyoamua!

Nembo ya Amnesty International
Nembo ya Amnesty International

Mfano juu ya mtu kupewa adhabu ya kifo kwa sababu tu ya kutazama tamthilia, unatoka Korea ya Kaskazini.

Hakuna mengi juu ya Korea ya kaskazini katika ripoti iliyotolewa mnamo mwaka huu ya Shirika la Kutetea haki za binadamu, Amnesty International.

Watu wanaendelea kunyongwa nchini humo.Huo ni ukweli.Lakini shirika la Amnesty international halina taarifa zinazoweza kuitia hatiani Korea ya Kaskazini

Hali ya adhabu ya kifo ilivyo Korea Kaskazini

Msemaji wa shirika hilo Ferdinand Muggenthaler ameeleza katika mahajiano na DW kwamba, ni vigumu kuhusu Korea ya Kaskazini kusema iwapo mtu ananyongwa kutokana na hukumu ya mahakama, au ni mauaji yanayofanywa na serikali au mtu anapotea tu.!

Kwa jumla shirika la Kutetea haki za binadamu la Amnesty International huchapisha zile takwimu katika ripoti zake za mwaka ambazo hutokana ama na vyanzo rasmi au idadi zilizothibitishwa kutokana na uchunguzi au kutokana na taarifa za jamaa wa walionyongwa.

Hakuna nchi inayojifungia ndani kama Korea ya Kaskazini. Lakini pia zipo nchi nyingine ambazo hazitoi taarifa juu ya adhabu za kifo zinazotolewa au juu ya hukumu za kifo zinazotekelezwa. Mfano ni China.

Kitanda kinachotumika katika adhabu ya kifo
Kitanda kinachotumika katika adhabu ya kifoPicha: picture-alliance /dpa/dpaweb

Kwa mujibu wa duru za kuaminika, maalfu ya watu wananyongwa nchini humo lakini habari juu ya watu hao zinafichwa na kwa hivyo idadi halisi haijulikani.

Ripoti ya Shirika la kutetea haki za binadamu Amnesty International inasema ongezeko la idadi ya watu walionyongwa mwaka jana duniani imetokana na adhabu za kifo zilizotekelezwa nchini Iran, Iraq na Saudi Arabia.

Marekani pia ni miongoni mwa nchi tano duniani ambako idadi kubwa ya watu walinyongwa. Shirika hilo pia limearifu hadi kufikia mwishoni mwa mwaka wa 2013 watu 23,000 duniani kote, bado walikuwa wanasubiri kunyongwa.

Mwandishi:Gessat,Michael

Tafsiri:Mtullya Abdu.

Mhariri: Gakuba Daniel