1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Afrika katika magazeti ya Ujerumani

Abdu Said Mtullya7 Desemba 2012

Magazeti ya Ujerumani wiki hii yaandika juu ya mgogoro wa mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo na uchaguzi wa Rais nchini Ghana.

https://p.dw.com/p/16xrF
Uchaguzi wa Rais nchini Ghana.
Uchaguzi wa Rais nchini GhanaPicha: picture-alliance/dpa

Gazeti la "Neues Deutschlanda" limeutupia macho uchaguzi wa nchini Ghana. Gazeti hilo linatilia maanani kwamba suala la utajiri wa mafuta ni muhimu katika uchaguzi huo.Linasema katika uchaguzi huo watu wa Ghana hasa wameangalia ni nani wanaweza kumwamini juu ya usimamizi mzuri wa utajiri unaotokana na mauzo ya mafuta.

Gazeti la "Neues Deutschland"linaarifu kwamba tokea neema kubwa ya mafuta ianze mnamo mwaka wa 2010 Ghana ilifikia ustawi wa asilimia 14 mwaka uliopita; kiwango cha juu kabisa duniani. Lakini gazeti la Neues Detchland" linatilia maanani kwamba theluthi moja ya wananchi wanaishi katika umasikini, na pamoja na hayo wengi hawajui kusoma na kuandika.
Gazeti hilo linafahamisha kwamba wakati katika mji mkuu,Accra,shughuli za kiuchumi zinastawi mtindo mmoja,wakati hali ya maisha siyo nzuri kaskazini mwa Ghana .Gazeti linasema ni katika sehemu hiyo kwamba Rais mpya atapaswa kuonyesha uwezo wake, kwani mpaka sasa watu wa sehemu hiyo bado hawajanufaika na ustawi wa uchumi.

Gazeti la "Süddeutsche Zeitung" pia limeandika maoni juu ya ustawi wa uchumi barani Afrika. Lakini limelifananisha bara hilo na Janus, Mungu wa kirumi mwenye sura mbili, moja mbele na nyingine nyuma.

Gazeti hilo linaeleza katika maoni yake kwamba bara la Afrika lina pande mbili. Katika upande mmoja maisha yananawiri,uchumi unastawi na baadhi ya watu wanasonga mbele katika maendeleo wakiwa na matumaini ya kuutokomeza umasikini.

Lakini katika upande mwingine bara la Afrika bado linakabiliwa na migogoro- ikiwa pamoja na vita. Hata hivyo gazeti la "Südeutsche" linasema katika maoni yake kwamba hali hiyo ya mikingamo pia inasaidia kutoa picha halisi ya Afrika.

Bara la Afrika linastawi pia kutokana na ushirikiano na China. Huo ni ukweli, hata ikiwa nchi za magharibi hazitaki kuukubali.
Ustawi huo unalijenga tabaka la kati ,magharibi na mashariki mwa bara la Afrika . Japo tabaka hilo linajekenga taratibu,litakuwa mbegu imara ya kuleta ustawi zaidi. Gazeti la "Südeutsche" linasema kila mtu anayo maoni yake juu ya sera za China barani Afrika, lakini ukweli ni kwamba China imezifungua macho nchi nyingi za Afrika.

Gazeti la "Die tageszeitung" wiki hii limechapisha taarifa juu ya hali ya mashariki mwa Jamhuri ya kidemokrasi ya Kongo baada ya waasi wa M23 kuondoka Goma.Lakini gazeti hilo linasema katika taarifa yake kwamba bado pana hali ya wasiwasi licha ya kuondoka kwa wapiganaji wa M23.

"Die tageszeitung" linaarifu ni polisi karibu 300 tu wanaolinda usalama na utulivu katika mji wa Goma.Polisi hao ndio wanaofanya doria barabarani,na ndio wanaolinda mipaka na Benki Kuu. Lakini katika sehemu nyingine za mji, kila mtu anaweza kufanya anachokitaka.

Katika taarifa yake, gazeti la "die tageszeitung"linafahamisha kwamba ,mara tu baada ya waasi wa M23 kuondoka katika mji wa Goma, watoto na vijana walizivamia kambi za kijeshi kwenye makao makuu ya jeshi katika Kivu ya kaskazini.

Mamilioni ya watoto wanatumikishwa kama vihongwe katika sehemu nyingi za dunia ikiwa pamoja na magharibi mwa Afrika. Gazeti la "Financial Times Deutschland" limechapisha makala juu ya utumwa huo wa watoto.Linaarifu kwamba wakati sikukuu za Kriskamasi zinakaribia, vitu vitamu kama vile chokleti zimejaa madukani barani Ulaya na kwingineko. Kiasi kikubwa cha chokleti kinatoka Afrika magharibi. Wanaofanya kazi ya kuvuna kakao ni watoto. Kwa mujibu wa shirika la biashara duniani WTO, watoto wengi wanafanyishwa kazi hiyo ya uvunaji kiasi kwamba wanashindwa kuenda shule. Nusu ya watoto hawaendi shule nchini Ivory Coast kutokana na kufanya kazi katika mashamba ya kakao nchi humo.Kutokana na hali hiyo, gazeti la "Financial Times Deutschland" linasema chokleti sasa inakuwa chungu.!

Mwandishi: Mtullya abdu.Deutsche Zeitungen:

Mhariri: Mohammed Khelef