1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Afrika katika magazeti ya Ujerumani

Zainab Aziz
22 Desemba 2017

Matukio ya barani Afrika yaliyozingatiwa na magazeti ya Ujerumani mnamo wiki hii.ni pamoja na makala ya gazeti la Berliner Zeitung inayozungumzia juu ya kupata nguvu kwa chama tawala cha nchini Afrika kusini ANC.

https://p.dw.com/p/2pqsi
Filmplakat The Court Dokumentation über den Strafgerichtshof in Den Haag

Kwa muda wa  zaidi  ya nusu mwaka chama cha ANC kilikuwa kinakabiliwa  na  mivutano  ya ndani  kuhusu uongozi.Lakini  mwanzoni mwa wiki iliyopita  chama  hicho kilimchagua  kiongozi  wake  mpya  Cyril Ramaphosa. Kuchaguliwa  kwake  kunazingatiwa kuwa  hatua muhimu ya kwanza  katika kuliwinga wingu la mfarakano lililokuwa limetanda juu ya chama cha ANC. Katika uchaguzi uliofanyika, Ramaphosa alimshinda Nkosazana  Dlamini Zuma alieiwakilisha kambi ya rais Jacob Zuma, anaetarajiwa  kuondoka madarakani mnamo  mwaka  2019. Gazeti la Berliner Zeitung  linatilia maanani  kwamba,

Kinyang‘anyiro cha kumtafuta  rais mpya  wa chama  cha ANC kilikuwa  baina ya  kambi ya Ramaphosa  na  ya Jacob Zuma  na ndiyo sababu huenda Ramaphosa akabililiwa na changamoto baada ya  kuahidi  kuleta  mageuzi  ya  kina ndani ya chama. Hatahivyo ushindi  wa Ramaphosa unazingatiwa kuwa muhimu sana katika muktadha wa uchaguzi mkuu  utakaofanyika mwaka 2019  nchini  Afrika Kusini. Kwa mujibu  wa  gazeti la Berliner Zeitung, endapo Dlamini  Zuma, aliekuwa mke wa Rais  Zuma angelimshinda Ramaphosa chama  cha  ANC kingelikuwamo  katika  hatari  kubwa  ya  kushindwa katika uchaguzi  huo  mkuu.

Cyril Ramaphosa makamu wa rais wa Afrika Kusini
Makamu wa rais wa Afrika Kusini Cyril RamaphosaPicha: Getty Images/AFP/G. Khan

Handelsblatt

Gazeti la masuala  ya  kibiashara, Handelsblatt pia linazungumzia juu ya hali ya nchini  Afrika Kusini  na linasema  kwamba nchi hiyo  inahitaji mwanzo mpya, na linaeleza. Afrika Kusini imekuwamo katika njia mrama. Lakini  baada  ya kuchaguliwa kiongozi mpya  wa  chama tawala ANC, Ramaphosa, masoko yanaweka matumaini juu  yake. Matumaini ni makubwa kwa sababu  Ramaphosa ni mfanya biashara aliefanikiwa na pia ni mtu mwenye ufahamu mkubwa juu ya masuala ya wafanyakazi. Hata hivyo gazeti la Handelsblatt linatahadharisha juu ya kumzingatia Ramaphosa kuwa mtu mwenye uwezo  wa kuleta miujiza.Pamoja na hayo  linakumbusha  kwamba mwanasiasa  huyo alikuwa makamu wa rais Jacob Zuma

die tageszeitung.

Gazeti la die  tageszeitung wiki hii linazungumzia  juu ya uamuzi wa  kihistoria uliotolewa na mahakama  ya kimataifa ya kupambana na uhalifu ya  mjini the  Hague.Gazeti hilo linaeleza mahakama ya kimataifa ya mjini The Hague sasa inautekeleza wajibu wake kwa uthabiti  wote. Taasisi hiyo ya kisheria iliamua wiki iliyopita  kwamba  waliokumbwa na uhalifu uliofanywa na mbabe  wa kivita Thomas Lubanga nchini Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Kongo walipwe fidia jumla ya dola milioni 10 na mhalifu huyo. Uamuzi huo umefungua  njia mpya pamoja na kuhukumiwa, wahalifu hao wanawajibishwa kutoa kifuta  machozi kwa  wahanga.

Mbabe  wa  kivita Thomas Lubanga aliekuwa  kiongozi  wa kundi la wanamgambo wa UPC (Union  of Congolese Patriots) aliongoza vita kwenye jimbo la Ituri, kaskazini mwa Jamhuri ya kidemokrasia ya Kongo kuanzia mwaka wa 2002 hadi  2003. Lubanga alitiwa hatiani na mahakama ya kimataifa kwa uhalifu wa kuwaandikisha watoto kupigana vita. Gazeti la die tageszeitung linaeleza kuwa watoto hao walidhulumiwa utoto wao kutokana na kuingizwa kwenye makundi ya wapiganaji.

Thomas Lubanga akiwa ICC The Hague 19.05.2014
Thomas Lubanga mbabe wa kivitaPicha: Reuters

Watoto hao walilazimishwa kuondoka makwao na kupelekwa vitani.Walinyanyaswa kwenye kambi  za kijeshi na walidhulumiwa fursa  za  kwenda shule.Hata hivyo gazeti la  die tageszeitung linatilia maanani kwamba uhalifu uliofanywa  na  watu  hao walipokuwa  askari watoto haukuzingatiwa na mahakama. Lakini wao ndio watakaolipwa fidia.

Gazeti la Die tageszeitung pia limeandika kuhusu biashara ya nguo kuu kuu maarufu kama mitumba, Bi Carol Nambuga anauza nguo hizo za zamani kwenye soko kubwa zaidi katika Afrika Mashariki -Soko la Owino, huko mjini Kampala. Lakini kuna hofu kwamba biashara hiyo inaelekea kufikia mwisho wake, kwa sababu Afrika inataka kuimarisha viwanda vyake vya kutengeneza nguo mpya. Die tageszeitung linasema hiyo ni fursa nzuri kwa wafanyabishara  wa Ujerumani.

Gazeti hilo linasema kila uchao, maelfu ya wauzaji wa mitumba kama vile Nambuga wanaendesha kazi zao kwenye soko hilo lililo kati ya eneo la biashara za rejareja na mitaa katika barabara za mji mkongwe uliopo mjini Kampala. Zaidi ya wafanyabiashara 50,000 wanashughulika katika eno hilo lenye ukubwa wa heka saba. Wengi, wao kama alivyo Nambuga, wana meza ya mbao au vigingi wanavyotumia kutundika bidhaa zao na ambazo hutumika kama maduka.

rais wa Uganda Yoweri Museveni
Rais wa Uganda Yoweri MuseveniPicha: Reuters/J. Akena

Baadhi ya wafanyabishara hao wa mitumba hubeba bidhaa zao mabegani kama vile sidiria, mifuko, mashuka, mikanda au vitambaa kama njia moja ya kuboresha biashara zao. Eneo hilo hushamiri kwa kelele kila mmoja akiinadi bidhaa yake kwa sauti. Lakini sasa, wafanyabiashara wengi katika soko hilo la Owino na masoko mengine kama hayo katika eneo la Afrika mashariki wanaogopa kupoteza ajira zao kutokana na viongozi wa Nchi za Jumuiya ya Mashariki ya Afrika kuamua manamo mwaka jana kuondokana na uagizaji wa mitumba hadi kufikia mwaka wa 2019.

Nchi za Afrika Mashariki kama Rwanda, Uganda,Tanzania na Kenya zitakuwa zinaongeza kodi kwa kila mwaka kwa bidhaa hizo zinapoagizwa. Lengo ni kuongeza mahitaji ya nguo zinazotengenezwa ndani ya nchi zao na hivyo kuweza kufufua sekta ya nguo katika kanda hiyo. Zaidi ya yote, hatua hii inalenga kuongeza nafasi za ajira. Katika mkutano wa biashara kati ya Ujerumani na bara la Afrika uliofanyika mjini Berlin, Rais wa Uganda Yoweri Museveni aliwahimiza wafanya biashara wa Ujerumani kuwekeza katika sekta ya nguo nchini Uganda nchi hiyo ikiwa ni mzalishashaji mkubwa wa pamba katika eneo la Afrika Mashariki.

Mwandishi: Zainab Aziz/Deutsche Zeitungen

Mhariri:Yusuf Saumu