1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Afrika Mashariki yalia na EU makubaliano ya EPA

8 Juni 2015

Kwa zaidi ya miaka 10, Umoja wa Ulaya ulifanya majadiliano na nchi za jumuiya ya Afrika Mashariki kuhusu makubaliano ya biashara huru - EPA. Kenya hasa haikutaka kusaini makubaliano hayo , lakini haikuwa na nguvu.

https://p.dw.com/p/1FdDp
Konferenz in Kampala
Picha: AP

Hii ni kwa sababu ingawa makubaliano hayo yanatoa fursa kwa mataifa ya Afrika Mashariki kuuza bidhaa zao katika soko la Ulaya bila kulipishwa kodi, Umoja wa Ulaya umeweka masharti magumu kwa mataifa hayo ambayo wachambuzi wanayaona kuwa ni unyonyaji.

Godfrey Ng'anga anafuga kuku wapatao1500 na Ng'ombe sita pembenzoni mwa mji wa Nairobi. Yeye hasa ni mkulima mdogo, kama walivyo malefu ya Wakenya. Lakini ana hofu kuwa nguvu ya soko la Ulaya inaweza kumsambaratisha.

"Walipaswa kununua bidhaa zetu kama vile maziwa, kuku, mayai na ng'ombe, lakini teknolojia yao ni ya juu sana na wanaweza kutuuzia bidhaa zao kwa bei nafuu sana kuliko sisi tunavyoweza kuuza kwao," alisema mkulima huyo katika mahojiano na DW.

Maua huiingizia Kenya fedha nyingi za kigeni hasa kutoka Umoja wa Ulaya.
Maua huiingizia Kenya fedha nyingi za kigeni hasa kutoka Umoja wa Ulaya.Picha: picture alliance/Photoshot

Sababu za hofu yake na wakulima wengi wadogo nchini Kenya ni makubaliano ya biashara kati ya Umoja wa Ulaya na jumuiya ya Afrika Mashariki EPA, yaliyosainiwa mwaka uliyopita. Makubaliano hayo yalipaswa kuleta tija kwa wote.

Lakini nchini Kenya, kila yanapotajwa makubaliano hayo, neno linalokuja akilini mwa watu "vitisho!" kwa sababu baada ya miaka kumi ya majadiliano na jumuiya ya Afrika Mashariki - ambayo inajumlisha mataifa ya Kenya, Rwanda, Tanzania na Uganda, Umoja wa Ulaya ulikuwa na shauku ya kusaini makubaliano hayo.

'Makubaliano mabaya kabisaa'

Serikali mjini Nairobi haikuridhika na haikuwa tayari kusaini makubaliano hayo - kutokana na hofu kwamba sekta yake ya kilimo ambayo ndiyo sekta muhimu zaidi ya kiuchumi isingeweza kuhimili ushindani na bidhaa za matunda na mbogamboga za bei nafuu na zenye ruzuku kutoka Umoja wa Ulaya.

Ingawa jumuiya ya Afrika Mashariki ina fursa ya kuuza bidhaa zake katika soko la Ulaya pasipo na kutozwa ushuru, Fredrick Njehu kutoka tume ya haki za binaadamu ya Kenya anayakosoa makubaliano hayo. "Ni makubaliano mabaya sana. Ukiangalia masharti uliyoyaweka Umoja wa Ulaya kwa jumuiya ya Afrika Mashariki, sioni kama watayamudu," alisema Njehu.

Taasisi ya masuala ya kiuchumi ya ndani, inakadiria kuwa tayari Kenya inapoteza zaidi ya euro milioni 100 kila mwaka kupitia makubaliano ya EPA, fedha ambazo zingesaidia kuchochea ukuaji wa kiuchumi.

Miongoni mwa mambo mengine, makubaliano ya EPA yanapiga marufuku utozaji wa kodi mpya kwa biadhaa zinazosafirishwa kwenda Umoja wa Ulaya ambazo umoja huo ungependa zipitie Afrika Mashariki, ili kuepusha kuathiri uchumi wake.

Mjumbe ya serikali ya Ujerumani kwa Afrika Guenter Nooke alikosoa mbinu za kibabe katika kujadili makubaliano ya biashara.
Mjumbe ya serikali ya Ujerumani kwa Afrika Guenter Nooke alikosoa mbinu za kibabe katika kujadili makubaliano ya biashara.Picha: DW/P. Henriksen

Bastola kifuani

Lakini kulingana na Umoja wa Ulaya, hofu hizi za mataifa ya Afrika Mashariki hazina msingi, kwa vile makubaliano ya EPA yananuwiwa kuimarisha ushirikiano. Na asiyetaka ushirikiano analaazimishwa kuukubali.

Kwa sababu kama Kenya, ambayo ndiyo chumi kubwa zaidi katika, ilipotaka kukataa kutia saini makubaliano ya EPA Oktoba mwaka jana, Umoja wa Ulaya uliamua kuibana kwa kuipandishia ushuru kutoka asilimia 8.5 hadi zaidi ya asilimia 30 kwa bidhaa zake kama vile maua, ambayo ndiyo moja ya bidhaa zinazouzwa nje kwa wingi, kahawa, nanasi za mkebe na chai.

Vitisho hivi, kama vinavoitwa nchini Kenya, vilikuwa na athari za haraka-na wiki chache baadaye, serikali ya Kenya pia ililaazimika kusaini makubaliano ya EPA. Mbinu hizi za kibabe za majadiliano zinakosolewa na wengi, akiwemo mjumbe wa serikali ya Ujerumani kwa Afrika Günter Nooke.

"Tunapeleka pesa nyingi za kodi katika program za maendeleo Afrika. Haifai kutumia makubaliano ya biashara kwa upande mmoja kuvunja yale tuliyojaribu kujenga kama wizara ya maendeleo kwa upande mwigine," alisema Nooke.

Hata baadhi ya wataalamu wa uchumi wa Umoja wa Mataifa hawaoni fursa yoyote kwa Afrika Mashariki na badala yake hata katika kipindi cha muda mrefu wanaona kitisho kwa jumuiya hiyo kupitia masoko ya Ulaya.

Mwandishi:Zierhut Jochen
Tafsiri: Iddi Ssessanga
Mhariri: Josephat Nyiro Charo