Al-Qaida yafurushwa Yemen
13 Juni 2012Hicho ni kifaru kikipita katika mji wa Jaar ambapo majeshi ya Yemen, yakisaidiwa na majeshi ya Marekani katika kikosi maalumu kilichopo Saudia Arabia, wameweza kuwatoa katika ngome zao katika miji hiyo na wanamgambo 30 wameuwawa na wengine kuanza kukimbia ovyo na kujificha katika vichaka vya milima jirani yalikofanyika mapigano hayo.
Akizungumza mmojawapo wa wakazi wa eneo la Jaar, Waleed Mohammed, amesema mapigano hayo yamefanyika kwa usiku kucha kwani walisikia milio ya kujibizana kwa risasi.
Mkazi huyu anasema walijua mapigano hayo yangedumu kwa mwaka mmoja kuweza kuiteketeza ngome ya Al-Qaida, lakini imekuwa kinyume kwani baada ya mapigano ya muda mchache waliwaona wakikimbia.
Shuhuda huyo ameongeza kuwa walichungulia kupitia madirisha ya nyumba zao baadae walionekana askari wenye sare zao wakipita mitaani kuonyesha kuwa sasa wanamgambo hao wa Al-Qaida wamefurushwa, hawapo katika mji wa Jaar.
Mafanikio ya kupambana na ugaidi
Ushindi huu unatanguliwa na mafanikio kadhaa ya kupambana na ugaidi kuanzia kuuwawa kwa kiongozi wa kundi hili, Osama Bin Laden, na kiongozi nambari mbili wa kundfi hilo, Abu Yahaya Al Libi, juni 4 mwaka huu.
Kunyakuliwa kwa miji ya Zinjibar na Jaar ni mafanikio makubwa. Hayo yanaungwa mkono na Brigedia Generali Mohammed al -Sawmali kutoka Jeshi la Yemen, lakini kiongozi huyo wakijeshi anasema kuwa kwa desturi ya makundi ya kigaidi lazima watajipanga tena na kutaka kurejea tena katika miji hiyo ambayo ilikuwa ni ngome yao hapo mwanzo.
Lakini kulingana na maandishi yaliyaoandikwa katika kuta za makazi ya watu katika miji ya Zinjibar na Jaar yanasomeka kuwa Al-Qaida haijashindwa vita bali imejiondoa katika miji hiyo.
Taarifa zinasema kuwa wakazi wa eneo hilo waliwaona wanamgambo wa kikundi hicho kama 500 wakiwamo watu kutoka mataifa mbalimbali wakikimbia huku wakipiga makelele na kusema hawajashindwa bali wanajiondoa wenyewe.
Maoni ya rais wa Yemen
Rais wa Yemen, Abed Rabbo Mansour, amesema kuwa lazima kikundi hicho cha kigaidi kinaondolewa katika ardhi ya Yemen.
Mwezi uliopita kikundi hicho kilikubali kuhusika katika mripuko wa kujitolea mhanga kwa askari waliokuwa katika mazoezi ya maandhimisho ya siku ya Muungano wa taifa hilo na kusababisha vifo vya askari zaidi ya100.
Mwandishi Adeladius Makwega APE/AFP
Mhariri: Miraji Othman