1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Al Sisi ashinda kwa kishindo uchaguzi wa rais Misri

29 Mei 2014

Kiongozi wa zamani wa jeshi Abdel Fattah al Sisi ameibuka na ushindi mkubwa katika uchaguzi wa rais nchini Misri. Amejikingia zaidi ya asili mia 90 ya kura lakini walioteremka vituoni inasemekana ni asilimia 44 tu.

https://p.dw.com/p/1C8rF
Wafuasi wa jemedari mstaafu al Sisi wanasherehekea ushindi wa kiongozi waoPicha: Reuters

Kiongozi huyo zamani wa jeshi, kwa mujibu wa duru za sheria amepata asilimia 93 nukta 3 ya kura wakati shughuli za kuhesabu kura zikiwa tayari zimekamilika. Mgombea Hamdine Sabahi, mpinzani pekee katika uchaguzi huo amepata asilimia 3 nukta 8 ya kura, huku asilimia 3 nukta 7 ya kuwa ikiwa ni kura zilizoharibika.

Lakini idadi ya walioshiriki kupiga kura ikadiriwa asilimia 44 nukta 4, kwa mujibu wa duru hizo na hivyo kuweka shaka kwenye uhalali wa Al- Sisi, muasisi wa mapinduzi yaliyomuondowa madarakani Julai mwaka jana rais aliyechaguliwa kidemokrasia Mohamed Morsi.

Yalipoanza kutangazwa matokeo ya uchaguzi, wafuasi wa Al Sisi walizunguka barabara za Cairo na kupeperusha bendera wakisheherekea ushindi wa mgombea wao, huku honi za gari zikisikia katika mji mkuu.

Usiku kucha wafuasi hao wa Jemedari mstaafu Sisi walijumuika wakiimba na kucheza kwenye eneo maarufu la Tahrir lililoshuhudia maandamano makubwa yaliyompinduwa aliyekuwa rais wa Msri, Hosni Mubarak Novemba 2011, baada ya kuiongoza Misri kwa zaidi ya miaka 30.

Sabbahi hafui dafu mbele ya Sisi

Televisheni ya Misri imeshatangaza Al Sisi kushinda kwa asilimia 96 nukta 2 ya kura baada ya kura kuhesabiwa kwa asilimia 90 ya vituo vya kupigia kura, ushindi uliopatikana baada ya kuwekwa kando wapinzani wote.

Kombobild Hamdien Sabahi und Abdel Fatah al-Sisi
Jemedari mstaafu al Sisi (kulia) na mpinzani wake SabahiPicha: picture-alliance/dpa

Jemedari huyo mstaafu ndiye aliyekuwa akiongoza serikali ya mpito aliyounda miezi 11 iliyopita baada ya kumpinduwa na kumtia jela Mohamed Morsi rais wa kwanza kuchaguliwa kidemokrasia katika nchi hiyo yenye idadi kubwa ya watu.

Al-Sisi amekuwa akikubalika kufuatia serikali ilivyo kuwa ikiyazima kwa umwagaji wa damu maandamano ya wafuasi wa Morsi.

Pia bwana Sabbahi aliyetajwa kuwa mpinzani hakuwa na meno makali dhidi ya Al-Sisi na kuonekana mbele ya macho ya wengi kama aliyepangwa tu kuwa na majukumu kama ya upinzani.

Wakati wa kampeni za uchaguzi huo, Al-Sisi alibaini kuwa na matumaini ya kupigiwa kura na zaidi ya milioni 45 ya wa Misri jumla ya milioni 54 wenye haki ya kupiga kura. Aibu kubwa kwake ilikuwa kuepusha kupata chini ya asilimia 51 nukta 85 kilopata chama cha Udugu wa kiislam Juni 2012 na kumuingiza Morsi madarakani.

Hali iliyopelekea tume ya uchaguzi iliyoteuliwa na serikali yake kurefusha kwa muda wa masaa 24 ya nyongeza kipindi cha kupiga kura kilichokuwa kimepangwa kwa muda wa siku 2, ambazo zilimalizika ikikadiriwa ni asilimia 37 peke ya waliopiga kura.

Uchaguzi na matokeo yake unawekewa suala la kuuliza

Tume hiyo ikileta hoja ya hali ya hewa, huku mashirika ya kutetea haki za binaadamu yakiuona uchaguzi huo kama "kichekesho" baada ya kutengwa upinzani ambapo wawakilishi wake walipigwa marufuku, au kufungwa aidha kuuwawa tangu kuondolewa madarakani Mohamed Morsi Julai 3 mwaka jana.

Präsidentschaftswahlen in Ägypten 28.05.2014
Honi zahanikiza Cairo kusherehekea ushindi wa al SisiPicha: Reuters

"Hakuna mtu nje ya Misri au katika mataifa ya magharibi aliyeamini kuwa ni uchaguzi huru na wa haki" alisema Shadi Hamid, mtafiti wa kituo cha Shaban, Marekani.

Kurefushwa kwa muda wa uchaguzi " utawala umeonekana kama usioweza, na hivyo kuwapa nguvu zaidi wafuasi wa Udugu wa kiislamu," aliongeza kusema. Wafuasi wa Udugu wa kiislamu waliotoa mwito wa kususia uchaguzi huo, walizungumzia asilimia 37 ya walioshiriki kupiga kura kama "kofi kali kwa utawala na kibali cha kifo cha mapinduzi ya Julai 3. "

Mwandishi/ Amida ISSA

Muhariri/Josephat Charo