1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

AMMAN: Kouchner ziarani Mashariki ya Kati

13 Septemba 2007
https://p.dw.com/p/CBQE

Waziri wa mashauri ya kigeni wa Ufaransa, Bernard Kouchner, amesema Ufaransa inamuunga mkono spika wa bunge la Lebanon, Nabih Berri katika pendekezo lake la kuvitaka vyama vya upinzani na vinavyoiunga mkono serikali vikubaliane juu ya mgombea mmoja wa urais.

Uchaguzi wa rais nchini Lebanon umepangwa kufanyika baadaye mwezi huu.

Akiwa mjini Amman nchini Jordan, waziri Kouchner ameonya juu ya uchaguzi wa rais nchini Lebanon kuingiliwa na nchi za kigeni na akaeleza matumaini yake kwamba uhuru na uhalali wa Lebanon utaheshimiwa. Aidha kiongozi huyo amesema Umoja wa Ulaya haujashawishika kwamba mpango wa nyuklia wa Iran ni wa matumizi ya amani.

Bernard Kouchner amezungumza na mfamle Abdulla II wa Jordan na rais wa mamlaka ya Palestina, Mahmoud Abbas kuhusu mkutano wa kimataifa wa amani ya Mashariki ya Kati utakaofanyika mwezi Novemba mwaka huu.

Akiwa katika ziara yake kwanza katika Mashariki ya Kati tangu uteuzi wake mapema mwaka huu, Kouchner ameondoka Jordan kwenda Misri.