1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

"Angela Merkel angefaa kukutana na Wapalestina"

Maja Dreyer2 Aprili 2007

Kansela wa Ujerumani, Bibi Angela Merkel, yuko ziarani katika nchi za Mashariki ya Kati. Je, wahariri wa magazeti ya humu nchini wanathamini vipi ziara hii?

https://p.dw.com/p/CHTM

Kwa ujumla, wahariri wanaona Angela Merkel habebi jukumu kubwa katika eneo hilo. Katika gazeti la “Kölnische Rundschau” tunasoma kwa mfano: "Kansela huyu hakufanya mazungumzo juu ya makubaliano ya amani, bali anatafuta njia tu kwa pande nne zinazoshughulikia amani katika Mashariki ya Kati, yaani Umoja wa Ulaya, Marekani, Urusi na Umoja wa Mataifa, zinaweza kuendeleza mazungumzo haya." Na gazeti hili linaendelea kusema kuwa Bi Merkel anajua ukweli wa mambo na amefahamu hatari kubwa ya mazungumzo haya kuvunjika haraka.

Gazeti la “Frankfurter Allgemeine Zeitung” linamkosoa Angela Merkel kwa kutochukua hatua ya kukutana na serikali ya Palestina, hasa baada ya nchi za Kiarabu kuimarisha mpango wake wa amani. Tunasoma: “Angela Merkel angefaa kuchukua hatua isiyo ya kawaida na ni ya kishujaa ikiwa angekutana na Wapalestina na hivyo kutathmini kama serikali hii iko tayari kubadilisha msimamo wake. Kwa kufanya hivyo, Angela Merkel, kwa kweli angeendeleza utaratibu wa amani.”

Mhariri wa “Berliner Zeitung” ameandika "Kwa hivi sasa hasa ni juu ya Marekani kuwakaribia Wapalestina na kuzungumza na chama cha Hamas. Ila tu tangu kuingia madarakani rais Bush sera za Marekani kuelekea Mashariki ya Kati zilikuwa mbaya sana. Kwa hivyo hadi baada ya Bush kumaliza muda wake kama rais, hapo tu ndipo Marekani inaweza kujitolea zaidi kwa amani kati ya Palestina na Israel."

Marekani imejiingiza katika mzozo mwingine, yaani ule kati ya Uingereza na Iran juu ya wanamaji hawa 15 walioshikwa na Iran. Bush alisema hii ni kesi ya utekaji nyara.

"Yule ambaye rafiki wa aina hiyo hana haja tena kuwa na maadui." Ni maneno yake mhariri wa Westdeutsche Allgemeine Zeitung”. Mhariri wake anachambua kwamba licha ya Rais Bush kusema ukweli, kwa kuikosoa wazi Iran aliathiri diplomasia kimya ya Uingereza na kuhatarisha uwezekano wowote wa kurudi haraka nyumbani wanamaji hawa 15.

Na haya yote yanatokea wakati leo hii tunakumbuka vita vya visiwa vya Falkland ambavyo vilianza miaka 25 iliyopita. Pale Uingereza ilielekea njia ya vita ili kuhakikisha visiwa hivi vibaki kuwa ardhi ya Uingereza.

Kwa mujibu wa gazeti la “Die Welt”, Uingereza haina matarajio kushinda vita dhidi ya Iran. Kwa hivyo, inaibidi serikali ya Blair kuimarisha juhudi zake za kidiplomasia. Gazeti hili lakini pia linachambua kuwa mzozo huu umeonyesha wazi hatari ya Iran na kuuliza: nini basi ingeweza kutokea ikiwa Iran itakuwa na silaha za kinyuklia. Kwa hivyo, gazeti lina hakika upinzani dhidi ya mradi wa kinyuklia wa Iran utakuwa mkubwa zaidi.