1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Assad kuhutubia taifa leo

Sekione Kitojo20 Juni 2011

Rais Bashar al-Assad wa Syria anatarajiwa kutoa hotuba muhimu leo ikiwa ni mara ya tatu tangu kuanza kwa maandamano ya kudai uhuru na mageuzi ya kidemokrasia nchini humo katikati ya mwezi Machi mwaka huu.

https://p.dw.com/p/11fI7
Rais wa Syria Bashar al-Assad anatarajiwa kutoa hotuba muhimu kwa taifa hilo leoPicha: AP

Hotuba hii inakuja baada ya wanaharakati wa upinzani kutangaza kuwa wanaunda baraza la taifa, ili kuratibu mapambano dhidi ya utawala wa Rais Assad.

Itakuwa ni mara ya tatu kwa Assad kutoa hotuba muhimu tangu maandamano yanayodai uhuru zaidi pamoja na demokrasia kuzuka nchini Syria katikati ya mwezi Machi 2011.

Jana Jumapili, majeshi ya Syria yaliingia katika eneo la mpaka wa kaskazini magharibi kuwazuwia raia wa nchi hiyo wanaokimbilia nchini Uturuki. Wanaharakati wa haki za binadamu wamesema kuwa maelfu ya raia ambao wamekuwa wakikimbia wamekwama na wafanyakazi wa mashirika ya kutoa misaada waliokuwa wakijaribu kuwapa chakula na mahitaji mengine wameshambuliwa na majeshi ya serikali.

Shambulio la hivi karibuni kabisa linafuatia maandamano makubwa nchini Syria siku ya Ijumaa, wakati wanaharakati wa haki za binadamu wanasema majeshi ya usalama yamewauwa waandamanaji zaidi ya 19.