1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Assad kulihutubia taifa leo kuhusiana na 'masuala ya ndani'

Mohammed Khelef10 Januari 2012

Rais Bashar Al Assad wa Syria anatarajiwa kulihutubia taifa hivi leo kuhusiana na masuala ya ndani ya nchi, ya kimataifa na ya eneo la Mashariki ya Kati, huku shinikizo na upinzani dhidi yake ukiongezeka siku hadi siku.

https://p.dw.com/p/13ghS
Rais Bashar Al Assad wa Syria.
Rais Bashar Al Assad wa Syria.Picha: picture-alliance/dpa

Hakuna undani zaidi wa hotuba hiyo uliotolewa, lakini hapo jana Waziri Mkuu wa Uturuki, Tayyip Erdogan, alisema kwamba nchi yake inatishwa na mgogoro unaoendelea nchini Syria na kwamba sasa itapaswa kuchukuwa jukumu la kuuzuia mgogoro huo. Uturuki ni jirani wa Syria na nyumbani kwa makumi kwa maelfu ya wakimbizi wa nchi hiyo wanaokimbia ukandamizaji wa serikali ya Assad. Erdogan amesema hali ya Syria inaelekea kwenye vita vya wenyewe kwa wenyewe.

Wakati huo huo, Jumuiya ya Nchi za Kiarabu imetangaza kuongeza idadi ya waangalizi wake nchini Syria kufikia 200 kutoka 165 waliopo sasa. Hata hivyo upinzani nchini Syria hauna imani na Jumuiya ya Kiarabu na unailaumu Jumuiya hiyo kwamba inazidi kuipa muda serikali ya Assad kuendelea na mauaji dhidi ya raia. Umoja wa Mataifa unasema kwamba hadi sasa watu 5,000 wameshauawa tangu maandamano dhidi ya Assad yaanze mwezi Machi mwaka jana.