1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Aubameyang aizamisha Hamburg SV

Sekione Kitojo
7 Novemba 2016

Pierre Emerick Aubameyang alipachika mabao manne Jumamosi (05.11.2016)wakati Borussia Dortmund ikiishindilia Hamburg SV  mabao 5-2, wakati viongozi wa ligi ya Bundesliga Bayern Munich ilitoka sare bao 1-1 na Hoffenheim.

https://p.dw.com/p/2SEfe
Fußball Bundesliga W10 HSV gegen BVB
Piere emerick Aubameyang akipongezwa na Piszcezek mlinzi wa Borussia DortmundPicha: picture-alliance/dpa/A. Heimken

Matokeo  katika  uwanja  wa  Allianz Arena  yana  maana  RB Leipzig ambayo  iko  katika  nafasi  ya  pili inaweza  kufikisha  pointi  sawa na  mabingwa  hao  watetezi, pointi 24  juu  ya  kilele  cha Bundesliga  iwapo  watashinda  nyumbani kwa  timu  iliyoko  katika nafasi  ya  kati  ya  Mainz 05  leo Jumapili,(06.11.2016).

Yalikuwa  matokeo  mazuri  kwa  Hoffenheim, ambayo  inaendeleza mwendo  wa  kutofungwa  hadi  sasa  msimu  huu  chini  ya  kocha mwenye  umri  wa  miaka  29 Julian  Nagelsmann.

Fußball Bundesliga FC Bayern München - TSG 1899 Hoffenheim
Wachezaji wa Hoffenheim wakishangiria bao dhidi ya Bayern MunichPicha: picture-alliance/dpa/A. Gebert

Lakini  siku  ya  jana  Jumamosi  ilikuwa  ya  Aubameyang , ambaye alijirudi   kutokana  na  matatizo  aliyojiletea  katikati  ya  wiki  kwa kufunga  mabao  safi wakati  Dortmund  iliposhinda  kwa  mara  ya kwanza   katika  michezo  mitano  ya  ligi na  kuchupa  hadi  nafasi ya  tano.

Aubameyang  alisimamishwa  kwa  muda  na  kocha  Thomas  Tuchel katika  mchezo  wa  Jumatano  ambao  Dortmund  ilishinda  kwa  bao 1-0  katika  mchezo  wa  Champions League  nyumbani  dhidi  ya Sporting Lisbon  baada  ya  kwenda  Milan kwa  ndege  ya  binafsi pamoja  na  marafiki  siku  ya  Jumatatu.

Deutschland Fußball Bundesliga Trainer Julian Nagelsmann
Kocha wa Hoffenheim Julian NagelsmannPicha: Getty Images/Bongarts/A. Grimm

Lakini  kila  kitu  kilionekana  kupata  msahama mjini  Hamburg wakati  mshambuliaji  huyo  raia  wa  Gabon  aliposherehekea  bao lake  la  kwanza  kwa  kumwendea  kocha  Tuchel  na  kumkumbatia kwa  vicheko.

Aubameyang acharuka

"Auba"  alihitaji  dakika  27  tu  kupachika  mabao  matatu  ya kwanza na  kufunga   bao  la  nne  katika  kipindi  cha  pili. "nilifanya  makosa na  ilibidi  kuomba  msamaha. Nilishasema  "samahani"  kwa  timu  na kocha,"  Aubameyanga  alikiambia kituo cha  televisheni  cha  Sky.

"Nilihitaji  kutoa  huduma  yangu  kwa  timu  nzima  na  kocha, ambae tunaelewana  sana."  Alifunga  bao  la  kwanza  la  Dortmund dakika nne  tu  tangu  kuanza  mchezo.

Huu ulikuwa  mchezo  mbovu  kabisa  kwa  Hamburg  na  sio kile ambacho  mchezaji  mkongwe  wa  zamani  wa   timu  ya  taifa  ya Ujerumani  Uwe Seeler  alivyopondelea  katika   siku  yake  ya kuzaliwa  akitimiza  miaka  80 , wakati  akishuhudia  klabu  yake ikikubali  kipigo  cha  nane  katika  michezo 10  ya  Bundesliga.

Deutschland Ehrenpreis der Bundesliga - Uwe Seeler
Mzee Uwe Seeler ametimiza miaka 80 katika siku yake ya kuzaliwa zawadi aliyopata ni kipigo kutoka DortmundPicha: picture-alliance/dpa/M. Gambarini

Mjini  Munich , Bayern walinyimwa  ushindi  mara  ya  sita  mfululizo na  timu  iliyoko  katika  nafasi  ya  tatu  ya  Hoffenheim , ambayo iliendeleza  rekodi  yake  ya  kutofungwa msimu  huu.

Kerem Demirbay  alipachika  bao  baada  ya  kupata  pasi  safi kutoka  kwa  Nadiem Amiri  katika  dakika  ya  16, lakini  bao  hilo halikudumu  muda  mrefu.

Mchezaji  wa  kati  wa  Hoffenheim  Steven Zuber  alijifunga mwenyewe  katika  dakika 34 wakati  Robert  Lewandowski  akisubiri katika  nguzo  ya  goli.

Baada  ya  kuishinda  Tottenham  Hotspur  ugenini  katika Champions League  katikati  ya  wiki , Bayer  Leverkusen  ilifanikiwa kupata  ushindi  wa  mabao 3-2  dhidi  ya  Darmstadt  kwa  magoli ya  Hakan Calhanoglu, Julian Brandt  na  Charles  Aranguiz.

Wolfsburg yazinduka

Wolfsburg  ilijitoa  kutoka  katika  eneo  la  kushuka  daraja  hadi nafasi  ya  13   baada  ya  ushindi  wa  mabao  3-0  huku kukinyesha  mvua  kubwa  dhidi  ya   wachezaji  10  wa  Freiburg wakati  mchezaji  wa  kimataifa  wa  Ujerumani  Mario  Gomez alifunga  mara  mbili  wakati Ricardo Rodriguez  alipachika  bao  kwa mkwaju  wa  penalti. wakati  huo  huo  kocha  wa  mpito Valerien Islamael atabakia  kuwa  kocha  mkuu  wa  VFL Wolfsburg  kwa  wakati  huu, klabu  hiyo  ya  Bundesliga  imesema  leo  Jumapili  baada  ya  ushindi  hapo  jana Jumamosi  wa  mabao 3-0 dhidi  ya  Freiburg.

Freiburg Fußball Bundesliga SC Freiburg vs VfL Wolfsburg Trainer Valerien Ismael Wolfsburg
Kocha wa mpito Valerien Ismael sasa anakuwa kocha wa kudumu kwa mudaPicha: Imago/Pressefoto Baumann

Magoli  ya  dakika  za  mwisho  kutoka  kwa  mchezaji  aliyetokea kutoka  benchi  akiwa  mchezaji  wa  akiba  Raul Bobadilla  na  Halil Altintop  yaliipata  Augsburg  ushindi  wa  mabao 2-0  dhidi  ya Ingolstadt.Na kocha  wa  timu  hiyo  ya  Ingolstadt Markus Kauczinski amefutwa  kazi  na  klabu  hiyo  leo Jumapili baada  ya   kipigo hicho, timu  hiyo  ikiwa  na  mwanzo  mbaya  kabisa  katika  ligi  ya  Bundesliga  msimu  huu, ikiwa  na  pointi 2  na  haijawahi  kushinda  hadi  katika  mchezo  wa  10.

Markus Kauczinski Trainer FC Ingolstadt
Kocha aliyetimuliwa na Ingolstadt Markus KauczinskiPicha: Imago/Krieger

Mchezo  wa  mwisho  jana  Jumamosi  ulikuwa  kati  ya  FC Cologne na  Eintracht  Frankfurt. FC Cologne  iliporomoka  hadi  nafasi  ya sita  baada  ya  kukandikwa  bao  1-0  na  Eintracht  Frankfurt, bao pekee  ilililofungwa  na  mchezaji  wa  kati Mijat Gacinovic dakika tano  baada  ya  mchezo  huo  kuanza.

Siku  ya  Ijumaa  Hertha  Berlin iliiogesha  Borussia Moenchengladbach  bila  sabuni  kwa  kuizaba  mabao  3-0, wakati Salom Kalou  alipopachika  mabao  yote  matatu  ikiwa  ni  mabao yake  ya  kwanza  tangu  mwezi Aprili  mwaka  huu.

Anthony Modeste  pamoja  na  Pierre Emerick  Aubameyang wanaongoza  ufungaji  mabao  katika Bundesliga , ambapo  kila mmoja  amepachika  mabao  11. obert  Lewandowski   wa  Bayern Munich anafuatia  akiwa  na  mabao 7. Vedad Ibisevic ana  mabao 6 na  Yunus Mali  wa  Mainz  ana  mabao 5.

Deutschland Fußball Bundesliga - 1. FC Köln vs. Hamburger SV
Mshambuliaji wa FC Cologne Anthony ModestePicha: picture-alliance/dpa/M. Becker

 

Loew  ateua chipukizi katika  Die Mannschaft

Kocha  wa  timu  ya  taifa  ya  Ujerumani  Joachim Loew  ametaja kikosi  chake  na  kuwaita  wachezaji  watatu  wapya  katika  kikosi hicho kwa  ajili  ya  pambano  la  kufuzu  kucheza  katika  fainali  za kombe  la  dunia  mwaka  2018  nchini  Urusi  dhidi  ya  San marino na  mchezo  wa  kirafiki  dhidi  ya  Italia.

Fußball Benjamin HenrichsDFB U21 Nationalmannschaft, Deutschland - Slowakei
Benjamin Henrichs wa Bayer Leverkusen ateuliwa katika kikosi cha Joachim LoewPicha: picture-alliance/augenklick/firo Sportphoto

Kijana  chipukizi  wa  Bayer  Leverkusen  Benjamin Henrichs, Yannick Gerhardt  mwenye  umri  wa  miaka  22  kutoka  VFL Wolfsburg  na  Serge Gnabry  aliyepata  medali  ya  fedha  akiwa  na timu  ya  taifa  ya  Ujerumani  katika  michezo  ya  Olimpiki , ambaye anaonesha  mchezo  safi  akiwa  na  kikosi  cha  Werder  Bremen wote  wamejumuishwa  katika  kikosi  cha  timu  ya  taifa.

Ujerumani  inasafiri  kwenda  San Marino   katika  pambano  la kufuzu  fainali  za  kombe  la  dunia  Novemba  11  kabla  ya kupambana  na  Italia  katika  mchezo  wa  kirafiki  mjini  Milan  siku nne  baadaye.

Grindel  rais  wa  DFB

Reinhard Grindel  alichaguliwa  tena  siku  ya  Ijumaa  kuwa  rais  wa shirikisho  la  kandanda  la  Ujerumani  DFB kwa  kipindi  kamili  cha miaka  mitatu baa ya  kuchukua  nafasi  ya  Wolfgang  Niersbach , ambaye  alijuzulu  mwaka  jana  kwa  kuhusika  na  masuala  ya kombe  la  dunia  mwezi  Aprili.

Deutschland 42. Ordentlicher DFB-Bundestag Reinhard Grindel
Rais wa Shirikisho la kandanda nchini Ujerumani DFB Reinhard GrindelPicha: picture-alliance/dpa/M. Schutt

Grindel  alipata  kura  zote  kutoka  kwa  wajumbe 258  katika mkutano  wa  DFB  mjini  Erfurt.

Grindel  mwenye  umri  wa  miaka 55 ana lengo  la  kuliweka  katika hali  ya  kisasa  zaidi  shirikisho  hilo  la  DFB  ambalo  ndio shirikisho  kubwa  kabisa  la  taifa  katika  mchezo  mmoja  duniani likiwa  na  wanachama   zaidi  ya  milioni  6.

Mageuzi  yanahitajika  kutokana  na  suala  linalozunguka  kombe  la dunia  mwaka  2006, ambapo  Ujerumani  ilikuwa  mwenyeji , hali inayoweka  kiwingu  katika  soka  la  Ujerumani.

Chelsea  kidedea

Kocha  wa  Chelsea  ya  Uingereza Antonio  Conte  amedai  kwamba timu  yake  inaweza  kuwa  bora  zaidi, licha  ya  kupata  ushindi wake  mzuri  zaidi  akiwa  kocha  wa  timu  hiyo  hadi  sasa, akiueleza  ushindi  wa  kikosi  chake  wa  mabao 5-0  dhidi  ya Everton  kuwa  ni mzuri  sana.

UEFA EURO 2016 Achtelfinale Italien vs. Spanien Trainer Antonio Conte
Kocha wa chelsea Antonio ContePicha: Getty Images/AFP/M. Medina

Pep Guardiola  alikiri  Manchester  City  inahitaji  kujenga  uwezo mkubwa  wa  kufunga  mabao  baada  ya  kutoka  sare  ya  bao 1-1 na  Middlesbrough.  Kikosi  cha  Guardiola  kilipiga  hatua  kubwa katika  medani  ya  ulaya  wakati  walipoirarua barcelona  kwa mabao 3-1  katika  Champions League  siku  ya  Jumanne.

Lakini  siku  nne  baadaye  City  wanaonekana  kuwa  wachovu baada  ya  kipindi  cha  kwanza  ambapo  walicheza  vizuri.

Mabingwa  wa  Afrika  hoi

Mabingwa  wapya  wa  Afrika  Mamelodi Sundowns  wameondolewa katika  kombe  la  ligi  la  Afrika  kusini  jana jumamosi baada  ya kupoteza  mchezo   wa  robo  fainali  kwa  njia  ya  penalti dhidi  ya watu 10  uwanjani   wa  kikosi  cha  Super Sport United.

Pambano  hilo  la  watani  wa  jadi  mjini  Pretoria  liliishia  kwa  sare ya  bila  kufungana  baada  ya  dakika  za  nyongeza  katika  uwanja wa  Lucas "Masterpieces" Moripe  na  SuperSport  waliwaangusha mabingwa  hao  watetezi kwa  mikwaju  3-1.

Gebreselassie  rais  wa riadha Ethiopia

Mkimbiaji  wa  mbio  ndefe Haile Gebreselassie alichaguliwa   kuwa rais  wa  shirikisho  la  wanariadha   nchini  Ethiopia  siku ya Jumamosi  baada  ya  kusema  mchezo  huo  nchini  mwake "umeingia doa" kwa  madai  ya  matumizi  ya  dawa zinazoongeza nguvu  misuli  na  alitaka , "kusafisha hali  hiyo".

Bingwa  mara  mbili  wa  Olimpiki  katika  mbio  za  mita 10,000 alipata  kura  15  katika  uchaguzi  uliowahusisha  viongozi  wa majimbo  wa  vyama  vya  riadha.

Äthiopien Athleten Addis Abeba PK Haile Gebreselassie Gezehegne
Haile Gebreselassie (katikati) achaguliwa rais wa shirikisho la riadha nchini Ethiopia Picha: DW/G.Tedla

Aliwashinda  wagombea  wengine  wawili , ikiwa  ni  pamoja  na  rais aliyekuwa  madarakani  Alebachew Nigusse  ambaye  hakugombea.

Haile  Gebreselassie  amechaguliwa  kwa  kipindi  cha  miaka minne.

Wakimbiaji  wanaokadiriwa  kufikia  50,000 , ikiwa  ni  pamoja  na bingwa  wa  mwaka  jana  Mkenya , wamejiandikisha  kushiriki  katika mbio  za  marathon  za  mjini  New York  leo  Jumapili(06.11.2016).

Mani Pacquiao

Manny Pacquiao  alionesha  kwamba  bado  anazo  nguvu  za kutosha kwa  kumtwanga  Jessie Vargas  katika  pambano  la mkanda  wa  WBO  siku  ya  Jumamosi, na hasimu  wake  Floyd mayweather  alikuwapo  kushuhudia   pambano  hilo akikaa  karibu kabisa  na  ulingo wa  pambano.

Las Vegas WBO Boxen Manny Pacquiao vs Timothy Bradley
Manny Pacquiao mpiganaji masumbwi kutoka Ufilipino (kushoto) Picha: Reuters/USA Today Sports/M. Rebilas

Pacquiao   ambaye , ambaye  anafikia  umri  wa  miaka  38 mwezi ujao, alimuangusha  chini Vargas katika   duru  ya  pili  wakati akielekea  kushinda  pambano  hilo  lililikuwa  la  upande  mmoja ambapo  ushindi  huo  unamruhusu  kunyakua  pia   taji  la  WBO uzito  wa  Welter  ambao  yeye  pamoja  na  Mayweather waliushikilia  hapo  kabla.

Ni  taji  pekee  ambalo Pacquiao  alilitema   wakati  aliposhindwa mwaka  jana  na  Mayweather  katika  pambano  lililoingiza  fedha nyingi  zaidi   katika  historia  ya   ngumi  za  kulipwa.

Mwandishi: Sekione  Kitojo

Mhariri: Mohammed  Dahman