1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

BAGHDAD: Majeshi zaidi ya Marekani yaingia Baquba

13 Machi 2007
https://p.dw.com/p/CCJY

Wanajeshi zaidi ya 700 wa Marekani wamewasili mapema leo mjini Baquba katika mkoa unaokabiliwa na hali mbaya ya usalama wa Diyala nchini Irak kujaribu kuzima machafuko yanayoendelea kaskazini mashariki mwa mji mkuu Baghdad.

Kikosi hicho kimewasili mjini humo kikitokea kaskazini mwa Baghdad wakati ambapo jeshi la Marekani linaendelea na operesheni yake ya kuudhibiti mji huo.

Ikulu ya Marekani imethibitisha uwezekano wa kuwaondoa wanajeshi wote wa Marekani walio nchini Irak kama mpango wake mpya hautafaulu kuleta utulivu nchini humo.

Rais wa Irak, Jalal Talabani, ameonya juu ya matamshi hayo yaliyochapishwa leo akisema kuondoka mwa majeshi ya Marekani nchini Irak kutasababisha nchi hiyo kutekwa na wanamgambo wa kishia na kikurdi.

Jenarali wa zamani katika jeshi la Marekani, John Abizaidi amesema kutoa mafunzo maalumu kwa vikosi vya Irak kutasiadia kuvishinda vita.

´Ndio maana njia ya kushinda vita hivi ni kutoa mafunzo kwa vikosi vitakavyokuwa na uwezo na hatimaye nadhani ipo haja ya kuondokana na idadi kubwa ya majeshi ya kigeni yanayodhibiti eneo hilo.´

Wakati haya yakiarifiwa, jeshi la Marekani nchini Irak limetangaza kwamba watu saba wametiwa mbaroni kwenye kiwanda cha kutengeneza aiskrimu kuhusina na mashambulio ya mabomu yaliyofanywa na watu wa kujitoa muhanga maisha dhidi ya mahujaji wa kishia mjini Hilla yaliyoua watu takriban 120.