1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

BAGHDAD: Rice achelewa kuondoka Irak

6 Oktoba 2006
https://p.dw.com/p/CD5Y

Mtu mmoja ameuwawa na wengine kadhaa wakajeruhiwa mapema leo wakati wa shambulio la bomu kaskazini mwa Baghdad. Bomu hilo liliripuka nje ya jenereta ya umeme katika wilaya ya Qahira na kuliteketeza.

Wakati huo huo maofisa wa usalama wa Irak wamegundua maiti zaidi katika maeneo mbalimbali mjini Baghdad. Duru za polisi zinasema maiti hizo zilikuwa na alama za mateso.

Habari kutoka Arbil kaskazini mwa Irak zinasema waziri wa mambo ya kigeni wa Marekani Condoleezza Rice ameondoka nchini humo leo baada ya ndege yake kucheleweshwa kwa sababu ya hitilafu za kiufundi.

Marubani wa ndege hiyo hawakuwa na uhakika juu ya usalama wa ndege hiyo na wakaitisha ndege nyengine iliyombeba Rice na msafara wake kuelekea kambi ya jeshi la Marekani nchini Uturuki ambako ndege yake rasmi iilikuwa inamsubiri.

Condoleezza Rice anatarajiwa kwenda London Uingereza kuhudhuria mkutano wa wanachama wa baraza la usalama unaozungumzia uwezekano wa kuutaka Umoja wa Mataifa uiwekee vikwazo Iran kwa mpango wake wa nyuklia.