1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bajeti ya gharama za kijeshi yapanda zaidi mwaka 2006

11 Juni 2007

Taasisi ya kimataifa inayoshughulikia masuala ya amani, yenye makao yake mjini Stockholm imesema kiwango cha matumizi ya kijeshi duniani kimeongezeka katika mwaka wa 2006 ikilinganishwa na miaka ya nyuma.

https://p.dw.com/p/CHCq
Picha: AP

Marekani inaongoza katika nchi zinazotumia kiasi kikubwa cha fedha kugharamia matumizi ya kijeshi.

Taasisi hiyo inasema mwaka uliopita dollar billioni 1,204 zilitumika duniani kote kugharamia matumizi ya kijeshi . Kiwango hicho kimeongezeka kwa asilimia 3.5 ikilinganishwa na mwaka 2005.

Kiwango hicho ni kikubwa kabisa ikilinganishwa na kipindi cha miaka 10 iliyopita hali ilikuwa tafauti.

Marekani ndio nchi inayoongoza katika kugharamia matumizi ya kijeshi ambapo mwaka jana nchi hiyo ilitumia dolla billioni 26 katika shughuli zake za kijeshi kati ya dollar billioni 39 kiwango kilichotumika duniani kote kugharamia matumizi hayo.

Marekani inawakilisha asilimia 46 ya bajeti ya matumizi ya kijeshi duniani nchi zingine nne zinazoongoza ni pamoja na Uingereza,Ufaransa,China na Japan ambapo kila mmoja inawakilisha asilimia 4 hadi 5.

Tathmini ya taasisi hiyo ya SIPRI inaonyesha nchi za Ulaya magharibi na Amerika ya Kati ndio eneo pekee zilizokuwa na kiwango cha chini cha matumizi ya kijeshi katika mwaka 2006.

Bajeti ya Urussi katika masuala ya kijeshi imepanda kwa kiasi cha asilimia 12 mwaka jana.

Mwelekeo huo wa Urussi ulianza kuonekana tangu mwaka 1998.

Katika eneo la Mashariki ya Kati haikuwa rahisi kupata kiwango kamili cha bajeti yake ya kijeshi lakini kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa Saudi Arabia ni nchi inayosalia kuwa bajeti kubwa katika suala la kijeshi ikifuatiwa na Israel na Iran.

Barani Afrika Algeria inaongoza ambapo mwaka jana ilitia saini mikataba ya kijeshi na Urussi inayogharimu dollar billioni 10.5

Katika upande wa Asia China imeipita Japan kwa kuwa na bajeti kubwa ya kijeshi na kuifanya nchi hiyo kushikilia nafasi ya nne katika nchi zinazoongoza kwa mwaka 2006.

Asia kusini India inaendelea kuongoza kuwa mtumizi mkubwa linapokuja suala hilo la kijeshi kwa mujibu wa taasisi ya SIPRI China na India zinawakilisha asilimia 40 ya matumizi ya kijeshi katika eneo hilo.

Urussi na Marekani ndio nchi zinazouza silaha kwa kiwango kikubwa kabisa kuanzia mwaka 2002 hadi mwaka 2006 huku China na India zikiwa wanunuzi wakubwa wa silaha duniani.

Nchi nyingine zinazotajwa kuwa wanunuzi wakubwa wa silaha za kijeshi ni Israel na Saudi Arabia na umoja wa falme za Kiarabu.