1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Baraza la Usalama la UN, laitisha mkutano wa dharura kuhusu Sudan Kusini

Admin.WagnerD20 Desemba 2013

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limeitisha kikao cha dharura hivi leo chenye lengo la kudhibiti vitendo vya umwagikaji damu vinavyoendelea nchini Sudan ya Kusini.

https://p.dw.com/p/1Adsp
Südsudan Süd Sudan Flüchtlinge Unruhen Juba
Wakimbizi katika eneo la Umoja wa Mataifa ambako kumefanyika mauwajiPicha: Reuters

Ripoti za hivi punde zikisema wanajeshi wa Uganda wameshapelekwa katika mji mkuu wa Juba.Yote yanajiri baada ya kuuwawa walinzi watatu wa amani wa Umoja wa Mataifa kutoka India. Ikiwa si zaidi ya miaka mitatu tangu kuundwa kwake taifa hilo changa kabisa duniani, tayari mapigano yanayoonekana kama yanafanyika kwa misingi ya kikabilia yameshasababisha vifo vya mamia ya watu wakiwemo walinzi watatu wa amani wa Umoja wa Mataifa.

Awali jana, kundi la vijana wenye silaha walivamia maeneo ya Umoja wa Mataifa mjini Jonglei na kuwajeruhi watu kadhaa. Katika hatua nyingine baadaye wanamgambo kama hao waliwalenga na kuwauwa wanajeshi watatu kutoka India.

Taarifa ya mwakilishi wa India katika Umoja wa Mataifa

Balozi wa India katika Umoja wa Mataifa, Asoke Mukerji, alithibitisha kutokea mkasa huo nchini Sudan ya Kusini mbele ya baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa. Huu ni mkasa wa kwanza wa mauwaji ya wahudumu wa Umoja wa Mataifa katika mapigano ya taifa hilo. Katika kikao cha jana jioni Balozi wa Pakistan katika umoja huo Masood Khan aliomba wajumbe wa mkutano wakae kimya kwa dakika moja ikiwa ishara ya kuwakumbuka waliowawa nchini Sudan ya Kusini.

UN-Sicherheitsrat Resolution zu Syrien Chemiewaffen 27.09.2013
Baraza la usalama la Umoja wa MataifaPicha: Reuters

Baraza hilo lilipanga kuanza mkutano wake wenye lengo la kujadili machafuko yanayoendelea katika taifa hilo asubuhi ya leo. Ndani ya Sudan na hasa katika mji wa Juba kazi ya dharura ya kuwanusuru raia ya wa kigeni wanaoishi nchini humo imeanza. Ndege na helkopta zimekuwa zikiwachukua raia wa Marekani, Uingereza, wafanyakazi wa mashirika ya misaada pamoja na Maafisa wa Umoja wa Mataifa kwa lengo la kuwanusuru na vurugu.

Onyo la Ban Ki-moon

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon ametaka kufanyike mazungumzo ya kisiasa ili kunusuru taifa hilo. Katika taarifa yake, kiongozi huyo wa Umoja wa Mataifa amesema hatma ya taifa hilo changa ipo katika mikono ya uongozi wake wa sasa ambao unapaswa kufanya kila liwezekanalo kudhibiti machafuko ambayo yatakuwa usaliti mkubwa kwa zile jitihada za muda mrefu za kutafuta uhuru wake.

Ban Ki-moon New York 27.09.2013 Overlay
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moonPicha: picture alliance/abaca

Naye Rais Barack Obama wa Marekani ameonesha wasiwasi wake kuhusu taifa hilo kwa kusema lipo katika muelekeo wa vita vya wenyewe kwa wenyewe kwa wakati huu ambapo takribani watu 500 wametajwa kuuwawa.

Kwa upande wake serikali ya Sudan Kusini imetangaza kwamba vikosi vyake vya usalama vimeweza kudhibiti hali tete ingawa jana jioni ilikiri kupoteza udhibiti wa mji wa Bor, miongoni mwa maeneo yenye idadi kubwa ya watu ambako milio ya risasi ilisika kwa kiasi kikubwa.

Mwandishi: Sudi Mnette/AP/AFP
Mhariri: Mohammed Khelef