1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bayern waanza kutayarisha mvinyo

18 Machi 2013

Bayern Munich wanaendelea kuvunja rekodi za Bundesliga na sasa wamesalia na ushindi wa mechi mbili pekee washinde taji la msimu huu wakati Eintracht Frankfurt wakiendelea kudorora.

https://p.dw.com/p/17zgK
Bayern Munich players celebrate a goal of Mario Gomez (covered) against Bayer Leverkusen during their German first division Bundesliga soccer match in Leverkusen March 16, 2013. REUTERS/Wolfgang Rattay (GERMANY - Tags: SPORT SOCCER) DFL RULES TO LIMIT THE ONLINE USAGE DURING MATCH TIME TO 15 PICTURES PER GAME. IMAGE SEQUENCES TO SIMULATE VIDEO IS NOT ALLOWED AT ANY TIME. FOR FURTHER QUERIES PLEASE CONTACT DFL DIRECTLY AT + 49 69 650050
FC Bayern München - Bayer Leverkusen am 16.03.2013Picha: Reuters

Frankfurt walishindwa magoli mawili kwa moja na VfB Stuttgart. Bayern wangali kileleni na pengo la pointi 20 baada ya ushindi wa magoli mawili kwa moja dhidi ya Bayer Leverkusen, wakati Frankfurt wakiwa katika nafasi ya nne bila kupata ushindi katika mechi zao sita za mwisho baada ya kushindwa nyumbani na Stuttgart.

Huo ndio uliokuwa ushindi wa kwanza wa Stuttgart baada ya kushindwa mechi nne za mwisho, ikiwa ni pamoja na kushindwa mara mbili dhidi ya Lazio katika Europa League. Sasa wako katika nafasi ya 12 kwenye ligi kabla ya kuwaalika mabingwa Borussia Dortmund Jumamosi hii. Kocha wa Frankfurt Armin Veh amnaye amehusishwa na klabu ya Schalke 04, amesema ataamua kuhusu hatima yake wakati wa kipindi hiki cha mapumziko kwa ajili ya mechi za kimataifa, lakini hajatia saini mkataba na vijana hao wa samawati. Borussia Moenchegladbach ilipata ushindi wa nyumbani wa goli moja kwa sifuri dhidi ya Hannover na kusonga hadi nafasi ya saba. Hanover wako katika nafasi ya kumi.

Baada ya kufungua msimu kwa rekodi ya ushindi wa mech nane, na kufungwa magoli manane pekee katika mechi zao 24 za kwanza katika Bundesliga, ambayo ni rekodi nyingine, Bayern wameweka rekodi mpya ya Bundesliga kwa kusajili ushindi wa 12 ugenini msimu huu nyumbani kwa Leverkusen. Bayern wameshinda 22 kati ya mechi zao 26 za Ligi na sasa wanahitaji tu kuwashinda Hamburg nyumbani Jumamosi ijayo, kisha washinde nyumbani kwa Frankfurt mnamo Aprili 6 na wanyanyue taji lao la 23 la Bundesliga.

Nuri Sahin na Robert Lewandoswki ni moto wa kuotea mbali katika mashambulizi ya Borussia Dortmund
Nuri Sahin na Robert Lewandoswki ni moto wa kuotea mbali katika mashambulizi ya Borussia DortmundPicha: picture-alliance/dpa

Nambari mbili kwenye Ligi Borussia Dortmund, waliwasambaratisha Freiburg kwa kuwalaza magoli matano kwa moja, kutokana na magoli mawili kila mmoja yao Robert Lewandowski na Nuri Sahin. Dortmund ambao watachuana na Malaga katika robo fainali ya Champions League walifanya mshambulizi katika uwanja wao wa Signal Iduna Park wakati Lewandowski akiweka rekodi mpya ya kufunga katika kila mechi kati ya nane za mwisho. Jurgen Klopp ni mkufunzi wa Dortmund

Schalke waliduwazwa magoli matatu kwa sifuri nyumbani kwa Nuremberg na wakaanguka katika nafasi ya tano, baada ya kubanduliwa nje ya Ligi ya Mabingwa wiki iliyopita. Ugusburg ambayo inakumbwa na kitisho cha kushushwa ngazi, ilisajili ushindi wake wa nne katika mechi zao kumi za mwisho na kuyaweka hai matumaini yao. Waliwafunga Hamburg goli moja kwa sifuri. Werder Bremen nao wakalazimisha sare ya magoli mawili kwa mawili dhidi ya wanaoshikilia mkia Greuther Fürth.

Kule Enlgand, mkufunzi wa Manchester United Alex Ferguson ameionya timu yake dhidi ya kuanza kusheherekea mapema wakiamini kuwa tayari wamenyakua taji la 20 la Premier League. United wako pointi 15 mbele kufuatia ushindi wao wa goli moja kwa sifuri dhidi ya Reading, baada ya Mabingwa watetezi Manchester City kuzidiwa nguvu na Everton kwa kufungwa magoli mawili kwa sifuri.

Manchester United tayari wanalinusa taji la Premier League, England
Manchester United tayari wanalinusa taji la Premier League, EnglandPicha: Reuters

Ferguson hata hivyo amekataa kupunguza kasi licha ya United kuwa katika nafasi ya kushidna taji. Chelsea waliwazaba West Ham United mabao mawili bila jawabu na kusonga katika nafasi ya tatu, mbele ya Tottenham Hotspur ambao walishindwa goli moja kwa sifuri na watani wao wa London Fulham, ambapo mshambuliaji wa zamani Dimitar Berbatov ndiye alifunga goli hilo la ushindi. Nambar tano Arsenal walishinda magoli mawili kwa sifuri dhidi ya Swansea na kusalia katika nafasi ya kuwinda tikiti ya kucheza Ligi ya Mabingwa.

Nchini Uhispania, Lionel Messi alifunga mara mbili katika ushindi wa Barcelona wa mabao matatu kwa moja dhidi ya Rayo Vallecano wakati wakiweka pengo lao la uongozi wa pointi 13 juu ya La Liga kukisalia na mechi kumi pekee. Mabingwa Real Madrid wani wa pili baada ya kutoka nyuma mara mbili na kuwashinda Real Mallorca mabao matano kwa mawili nyumbani. Atletico Madrid wako nyuma na pengo la pointi moja katika nafasi ya tatu baada ya kuwazidi nguvu Osasuna kuwafunga magoli mawili kwa sifuri.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/Reuters/DPA/AP

Mhariri: Mohammed Khelef