1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

BEIRUT : Hizbollah na Syria yatupilia mbali madai ya Marekani

2 Novemba 2006
https://p.dw.com/p/CCwv

Hizbollah hapo jana imekanusha tuhuma za Marekani kwamba inataka kuipinduwa serikali ya Lebanon na spika wa bunge la Lebanon ambaye ni mshirika wa kundi hilo ameelezea mashaka yake juu ya dhamira ya Marekani kwa taarifa hizo.

Akizungumza kwenye televisheni ya Al Arabiya msemaji mkuu wa Hizbollah Hussein Rahhal ameishutumu serikali ya Marekani kwa kuingilia kati siasa za Lebanon kwa kujaribu kuipa nguvu serikali ya Waziri Mkuu Fouad Saniora.Amesema inachotaka Hizbollah na washirika wake ni serikali ya umoja wa kitaifa nchini Lebanon.Syria pia imetupilia mbali madai hayo ya Ikulu ya Marekani kuwa ni kichekesho na hayana msingi kwamba nchi hiyo imekula njama na Iran na Hizbollah kuipinduwa serikali ya Lebanon.

Msemaji wa Ikulu ya Marekani Tony Snow ametowa madai hayo pamoja na kusema kwamba Syria ilikuwa imejaribu kuzuwiya kuundwa kwa mahkama ya kimataifa kuchunguza mauaji ya waziri mkuu wa zamani wa Lebanon Rafik Hariri.

Kiongozi wa Hezbollah Sheikh Hassan Nasrallah ametishia kuitisha maandamano iwapo dai lake la kupatiwa theluthi moja ya viti vya baraza la mawaziri katika serikali ya Lebanon halitotimizwa jambo ambalo litaipa Hezbollah haki ya kura ya turufu juu ya maamuzi ya sera.