1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

BEIRUT: Wanajeshi watatu wa Lebanon wauwawa

18 Juni 2007
https://p.dw.com/p/CBqX

Wanajeshi watatu wa Lebanon wameuwawa leo kwenye mapigano makali kati ya jeshi la Lebanon na wanamgambo wa kundi la Fatah al Islam yaliyozuka tena katika kambi ya wakimbizi ya Nahr el Bared kaskazini mwa Lebanon.

Kwa mujibu wa afisa wa jeshi ambaye hakutaka jina lake litajwe, wanajeshi kadhaa wamejeruhiwa kwenye mapambano hayo ya leo.

Mapema leo vikosi vya jeshi la Lebanon viliwashambulia kwa mabomu wanamgambo wa Fatah al Islam walio ndani ya kambi hiyo.

Wakisaidiwa na vifaru na silaha nzito, wanajeshi wa Lebanon walizishambulia pia ngome za wanamgambo hao ndani ya kambi ya Nahr el Bared iliyo katika viunga vya mji wa bandari wa Tripoli, huku mapambano yakiingia wiki yake ya tano.

Walioshuhudia wanasema mashambulio ya mabomu ya jeshi la Lebanon yemesababisha moshi mweupe na mweusi kutanda kwenye anga ya eneo hilo na kuzusha moto kwenye majengo kadhaa ndani ya kambi hiyo ya wakimbizi.