1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

BEIRUT:Waziri mkuu atoa wito wa mazungumzo na Hezbollah

7 Desemba 2006
https://p.dw.com/p/CClp

Waziri mkuu wa Lebanon Fuad Siniora anatoa wito kwa kundi lililo na msimamo mkali la Hezbollah kurejea katika mazungumzo na serikali.Kulingana na kiongozi huyo maandamano hayatasuluhisha chochote katika matatizo ya kisiasa yanayokumba nchi hiyo.

Bwana Siniora aliyasema hayo kupitia tangazo la televisheni akiwa afisini mwake iliyo na ulinzi mkali.Maandamano hayo yanayolenga kuondoa uongozi ulioko madarakani yameingia siku yake ya sita sasa.

Wakati huohuo kanisa la kikatoliki la Maronite lililo na ushawishi mkubwa nchini Lebanon linaonya kuwa tatizo hilo la kisiasa limefikia pahali pabaya na kutoa wito kwa bunge kukutana ili kupata suluhu.Kanisa hilo aidha linatoa wito wa kuundwa serikali mpya vilevile uchaguzi wa rais kufanyika mapema.

Kwa upande mwengine Rais Emille Lahoud alipinga hapo jana wito wa kufanyika uchaguzi wa mapema wa rais.Kiongozi huyo anashikilia kwamba uundaji wa serikali ya kitaifa ndio suluhu kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na afisi yake.