1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

BEIT HANOUN: Wanawake 2 wa Kipalestina wameuawa na vikosi vya Israel

4 Novemba 2006
https://p.dw.com/p/CCwH

Wapalestina 19 wameuawa siku ya Ijumaa katika Ukanda wa Gaza,Israel ikiendelea na mashambulio yake katika eneo hilo.Si chini ya wanawake 2 waliuawa baada ya vikosi vya Kiisraeli kulifyatulia risasi kundi la wanawake wa Kipalestina.Wanawake hao waliitikia wito uliotolewa katika redio ya eneo hilo,kwenda kuwakinga wanamgambo waliojificha ndani ya msikiti kaskazini mwa Ukanda wa Gaza.Watu darzeni kadhaa walioshukiwa kuwa wanamgambo walifanikiwa kutoroka msikitini katika mji wa Beit Hanoun, uliovamiwa na vikozi vya Israel tangu siku ya Jumatano.Marekani imesema inasikitishwa na vifo vya watu wasio na hatia lakini imesema,mapigano hayo yamechochewa na mashambulio ya makombora yanayofanywa na Wapalestina.Rais Mahmoud Abbas wa Palestina tena ametoa wito kwa jumuiya kimataifa kuingilia kati kukomesha mmuagiko wa damu.Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa,Kofi Annan ameeleza wasi wasi wake kuhusu hali ya sasa katika Ukanda wa Gaza.Akizungumza mjini New York amesema kwa sababu ya machafuko yanayoendelea ni vigumu kupata amani ya haki na kudumu katika eneo hilo.