1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Benitez achukua usukani Real Madrid

4 Juni 2015

Aliyekuwa kocha wa klabu ya Italia ya Napoli Rafa Benitez ametangazwa rasmi kuwa kocha wa miamba wa kandanda Uhispania Real Madrid katika mkataba wa miaka mitatu.

https://p.dw.com/p/1FbXw
Fußball UEFA Europa League SSC Napoli - Dnjepr Dnjepropetrowsk
Picha: Getty Images/F. Pecoraro

Benitez mwenye umri wa miaka 55 amechukua mikoba ya Carlo Ancelotti ambaye aliondoka katika kilabu hiyo mwaka mmoja tu baada ya kuisaidia kushinda kombe lao la kumi la Ligi ya vilabu bingwa Ulaya – Champions League.

Benitez ambaye ni mzaliwa wa Madrid amehudumu misimu miwili kama mkufunzi wa Napoli, baada ya kuviongoza vilabu kadhaa vya Ulaya.

Baada ya kuisaidia Valencia kushinda kombe la Uefa mwaka 2004, mwaka uliofuatia alielekea Liverpool na kuisaidia kilabu hiyo kushinda kombe la vilabu bingwa Ulaya katika msimu wake wa kwanza katika kilabu hiyo ya Mersyside.

Miaka miwili baadaye aliisaidia Liverpool kufika katika fainali za kombe la vilabu bingwa Ulaya na mwaka 2013 alikuwa kaimu mkufunzi wa Chelsea waliposhinda kombe la Europa

Mwandishi: Bruce Amani/AFP
Mhariri: Charo Josephat