1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bremen na Munich uwanjani leo:

27 Februari 2009

Nani atatamba na nani atateleza ?

https://p.dw.com/p/H2Xp
W.Bremen yaikaribisha leo B.Munich.Picha: AP

Mabingwa wa Ujerumani Bayern Munich, wanateremka uwanjani kesho jumapili kupambana na mahasimu wao Werder Bremen huku timu zote mbili zikiwa zimetoa salamu kwa mwenzake kati ya wiki:Munich iliizaba Sporting Lisbon mabao 5-0 katika champions League wakati Bremen ilitimua AC Milan ya Itali nje ya Kombe la Ulaya la UEFA.

Huko Bouake,Ivory Coast,kinyanga nyiro cha Kombe la Afrika la mataifa kinaendelea huku Tanzania -Taifa Stars wakiwa na miadi jioni hii na Chipolopolo-Zambia.

Ushindi wa kishindo wa Bayern Munich katika champions League juzi wa mabao 5-0 dhidi ya Sporting Lisbon ya Ureno, umewanyamazisha vinywa wakoasoaji wa kocha Jurgen Klinsmann alao hadi leo ,kesho mabingwa hao wa Ujerumani wakikutana na Bremen huko Bremen,mambo huenda yakawa mengine.Klinsmann amekuwa akitiwa shindo mno baada ya Munich kulazwa mara tatu katika Bundesliga na zaidi jumamosi iliopita ilipofedhehewa tena nyumbani munich na FC Cologne.

Werder iko kati kati ya ngazi ya Ligi na ikipepesuka pia msimu huu kama Munich ,lakini kwa kuingoa meno AC Milan juzi katika Kombe la UEFA, Bremen na jogoo lao la Peru Claudio Pizzaro, alietia mabao 2 katika lango la AC Milan, huenda wakawapa Munich kibarua kigumu. Macho yote ya mashabiki wa Bundesliga kwahivyo, yatakodolewa Bremen hapo kesho.

Viongozi wa Bundesliga Hamburg walicheza pia kati ya wiki katika kombe la Ulaya la UEFA kabla mkutano wao kesho na Wolfsburg.Kocha wa Hamburg Martin Jol, amewasamehe mastadi wake 2 Albert Streit na Jerome Boateng kwa kupapurana wakati wa mazowezi.Awali walifungiwa kucheza.

Hoffenheim, chipukizi waliozusha maajabu ya dimba msimu huu wakiwa pointi 2 nyuma ya viongozi Hamburg, wana miadi na Borussia Dortmund.Frankfurt yaumana na Schalke wakati Leverkusen, inaitembelea Hannover.Berlin inatamba nyumbani mbele ya Borussia Moenchengladbach.Jana ijumaa, duru hii ya mwishoni mwa wiki hii, ilifunguliwa kwa changamoto kati ya FC Cologne Armenia Bielefeld.

Katika Premier League, jioni hii ni "kufa kupona" kwa Liverpool kwani ,ushindio dhidi ya Middlesbrough tu, ndio utakaowabainisha mabingwa Manchester United kwamba kinyanganyiro cha premier League mwaka huu bado hakijamalizika.Chelsea wakiwa pointi 3 nyuma ya Liverpool na nafasi ya 3 ,sasa wameanza kupata nguvu tangu kuangukia mikononi mwa kocha mdachi guus Hiddink na wana miadi na Wigan athletic.Arsenal wana miadi na fulham katika Emirates Stadium.

Katika Kombe la Afrika la mataifa ya wachezaji wasiocheza ngambo huko Abidjan na Bouake,Ivory Coast, Taifa Stars-Tanzania, itajaribu leo kukwepa risasi za Chipolopolo -Zambia baada ya juzi kuwatoa wenyeji Ivory Coast nje ya mashindano kwa bao 1:0.