1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bundesliga huenda ikampata mbabe Jumamosi hii

29 Aprili 2011

Ligi ya kabumbu ya Ujerumani Bundesliga inayokaribia ukingoni leo huenda ikampata mbabe wake, duru mbili kabla ya kumalizika kwa ligi hiyo.

https://p.dw.com/p/116aZ
Washabiki wa Dortmund wakiota ubingwa wa BundesligaPicha: AP/dapd

Borussia Dortmund hii leo huenda ikatawazwa kuwa mabingwa wapya , iwapo itashinda pambano lake nyumbani na Nuremberg, lakini pia ikiomba mungu Bayer Leverkusen ipoteze au itoke sare katika mechi yake na FC Cologne mjini Cologne.

Borussia Dortmund inaongoza kwa pointi tano zaidi ya Bayer Leverkusen inayokamata nafasi ya pili na iwapo itashinda hii leo mwanya utakuwa pointi nane, lakini kama Leverkusen watafungwa, ama ikitoka sare mwanya utakuwa pointi saba ambazo hakutakuwa na timu itakayoweza kuzifikia katika mechi mbili zitakazosalia hivyo Dortmund watatawazwa mabingwa wapya wa Bundesliga

Mlinda mlango wa timu hiyo Roman Weidenfeller amesisitiza kuwa hawana chochote cha kuhofu kuhusiana na mechi hiyo ya leo.

Dortmund wiki iliyopita katika matokeo ambayo hayakutarajiwa ilichapwa bao moja kwa bila na timu inayokamata nanga ya ligi hiyo Borussia Moenchengladbach.

Washabiki wa timu hiyo wiki hii walitoa kitisho kwa kuandika maandishi kwenye uwanja wa mazoezi wa timu kuwa watawapiga hadi kuwaua wachezaji iwapo timu itashuka daraja.Kocha wa Levekusen Jupp Heynckes anafahamu ugumu wa mpambano huo.

Trainer Jupp Heynckes
Kocha wa Bayer Leverkusen Jupp HeynckesPicha: dapd

´´Hili ni pambano la timu za eneo moja yaani Derby na ni pambano ambalo lina msisimko wa aina yake tofauti na mengine, na iwapo hapo kabla kuna maumivu au la kutokana na mabadiliko ya kocha.Kuna kitu fulani ambacho ni maalum kuhusiana na pambano hili.Na timu zote mbili ziko imara na kuhamasika kwa kiwango cha juu´´

Kwa upande mwengine kivumbi kiko kwa mabingwa watetezi Bayern Munich ambao kwa kweli wamekwishautema Uchampion huo na kilichobakia kwao hivi sasa wanapambana kupata nafasi ya tatu na kucheza katika ligi ya mabingwa barani Ulaya.

Bayen Munich wanapigana kumbo katika kuwania nafasi hiyo na Hanover 96 ambayo ndiyo inayoshikilia nafasi hiyo kwa sasa ikiwa pointi moja mbele ya Bayern Munich.

Bayen leo usiku wanapambana na Schalke, huku Hanover wakiwa nyumbani kuwakaribisha wakamata nanga Borussia Moenchengladbach.Nahodha wa Munich Philipp Lahm amesema bado ana imani kuwa wataipata nafasi hiyo.

Philipp Lahm
Philipp Lahm akipiga kwanja katika moja ya majukumu yake ya ulinzi Bayern MunichPicha: AP

´´Ni lazima tujiangalie, lazima tuchukue pointi zote tisa katika mechi zote tatu za mwisho.Na baadaye tusubiri kuona nini Hannover watakifanya.Naamini bado tumaini lipo ya kwamba hawawezi kushinda mechi zote tatu.Na tukifanya hivyo, basi tutakuwa tumefuzu kwa ligi ya mabingwa.Lakini tunachohitaji hapo ni lazima kuwajibika sote kwa pamoja kwa asilimia 100´´

Mechi nyingine za Bundesliga Jumamosi hii ni kati ya Hamburg na Freiburg, huku Hoffenheim ikiwaalika nyumbani Stuttgart.

Mwandishi:Aboubakary Liongo/Reuters/DPA/ZPR

Mhariri:Othman Miraji