1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Bunge la Marekani latishia kumwajibisha Mwanasheria Mkuu

Mohammed Khelef
2 Mei 2019

Kamati ya Sheria ya Bunge la Marekani imetishia kumchukulia hatua za kinidhamu mwanasheria mkuu, baada ya kukataa kwake kuhudhuria mbele ya kamati hiyo kutoa ushahidi wa ripoti ya mchunguzi maalum, Robert Mueller.

https://p.dw.com/p/3HpPG
USA Mueller Bericht l US-Generalstaatsanwalt William Barr vor dem Justizausschuss des Senats
Picha: Getty Images/A. Wong

Mwenyekiti wa kamati hiyo ya sheria ya Bunge la Marekani, Jerry Nadler, aliliarifu bunge kwamba Mwanasheria Mkuu William Barr alikuwa amekataa kuhudhuria kwenye kikao hicho licha ya kwamba wao, kama kamati, walijaribu vya kutosha kuyashughulikia yale ambayo mwanasheria huyo aliyaona kuwa ni mapungufu kwenye kikao cha jana yake (Mei Mosi), ambacho alibanwa vikali kuhusu namna alivyoitendea ripoti ya mchunguzi maalum, Robert Mueller.

Mwenyekiti huyo wa kamati ya sheria alimtaka Barr kutimiza matakwa ya kamati hiyo na kuitoa ripoti kamili ya Mueller juu ya Urusi, akionya kuwa endapo Barr hakufanya hivyo, basi bunge lingemtia hatiani kwa kulidharau na kulizuwia kufanya kazi yake, akisema tabia hiyo ya utawala wa Trump haipaswi kuvumiliwa:

"Kila mjumbe wa kamati hii, awe Democrat au Republican, anapaswa matokeo mabaya ya pale mjumbe wa serikali anaposema atadharau wito halali wa bunge. Wakiachiliwa bila kudhibitiwa, kitendo hiki cha utovu wa nidhamu dhidi ya bunge kitafanya iwe vigumu kuiwajibisha serikali au kutunga sheria ambayo inazuwia ukosefu wowote wa heshima kwa chombo hichi." Alisema Nadler mbele ya kamati hiyo.

Miito ya kujiuzulu

Jerry Nadler US-amerikanischer Politiker
Mwenyekiti wa Kamati ya Sheria ya Bunge la Marekani, Jerry Nadler.Picha: picture-alliance/newscom/K. Dietsch

Kukataa huku kwa mwanasheria mkuu kufika mbele ya kikao cha bunge kumetafsiriwa na wengi kwamba ni ishara ya utawala wa Trump kudharau muhimili huu muhimu wa nchi na hivyo miito imeanza kutolewa kumtaka Barr ajiuzulu.

Mmoja kati yao waliotoa kauli hiyo ni makamo wa zamani wa rais, Joe Biden, ambaye alisema Barr anajifanya kuwa zaidi mwanasheria wa Rais Trump badala ya kuwa mwanasheria wa nchi.

"Nadhani anapaswa kujiuzulu. Huyu si mwanasheria wa rais. Ni mwanasheria wa watu. Anapaswa kuwalinda watu na kuilinda katiba. Hajawekwa pale kumlinda rais anapofanya jambo lisilo sahihi." Biden alikiambia kituo kimoja cha televisheni alipoulizwa kuhusu hatua hii ya Barr.

Hata hivyo, baadhi ya wajumbe wa Republican kwenye kamati hiyo ya sheria walimtetea mwanasheria mkuu huyo, wakisema alitendewa vibaya kweli na wabunge waliombandika maswali ya kumdhalilisha na kumvunjia heshima, na hivyo ana haki ya kukataa kuhudhuria kikao ambacho kina muelekeo wa udhalilishaji, hasa kwa kuwa wajumbe wa Democrat wanasisitiza kuwa mwanasheria huyo akubali kuhojiwa pia na wanasheria wengine wa kawaida nje ya bunge.

Uamuzi wa Barr kukataa kuhudhuria mbele ya kamati ya sheria ulikuja ikiwa ni siku moja sio tu baada ya wizara yake kushindwa kuwasilisha mbele ya kamati hiyo ripoti kamili isiyohaririwa ya Mueller kama ilivyotakiwa na bunge.

AP, Reuters