1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

CAF yachukua tahadhari kuhusu Ebola

28 Agosti 2014

Mlipuko wa Ebola unaolitikisa eneo la Afrika Magharibi, unaendelea kuzusha hofu kubwa kote ulimwenguni wakati juhudi zikifanywa ili kudhibiti kitisho cha kusambaa virusi vya ugonjwa huo.

https://p.dw.com/p/1D2sV
Meneja wa Mawasiliano wa Shirikisho la Kandanda Afrika - CAF, Erick MwanzaPicha: CAF

Na Shirikisho la Soka Barani Afrika CAF limeelezea khofu kuhusiana na hali hiyo ambayo imeathiri baadhi ya michezo ya kandanda barani humo. Guinea sasa itachezea mchuano wake wa nyumbani wa kufuzu katika Dimba Kombe la Mataifa dhidi ya Togo nchini Morocco, baada ya kulazimika kuuhamisha katika uwanja mwingine kufuatia kitisho cha Ebola. CAF imesema mchuano huo wa kundi E utachezwa mjini Casablanca Septemba 5. CAF ilizipiga marufuku Guinea na Siera Leone dhidi ya kuandaa mechi zozote za kimataifa hadi katikati ya mwezi Septemba.

Sierra Leone bado haijapata mahali pa kuchezea mechi yake, kwa sababu ombi la kuutumia mji mkuu wa Ghana, Accra, halijakubaliwa, hali inayowaweka katika hali ya sintofahamu wakati wakijiandaa kuanza hatua yakufuzu katika makundi kwa ajili ya dimba hilo linaloanza mwezi JANUARI nhcini Morocco.

Msemaji wa CAF, Eric MWANZA anasema hatua waliyochukua dhidi ya Guinea na Sierra Leone siyo adhabu bali tahadhali "Tulichofanya kwa kuhamisha mechi kutoka nchi hizi, ambayo siyo adhabu bali hatua za kushirikiana na serikali zote katika kupambana na hali hii kwa sababu Ebola ni kitisho ulimwenguni kote. Tumeimarisha usambazaji wa habari kwa sababu ukosefu wa habari umekuwa mojawapo ya matatizo ambayo huenda yanachangia katika kusambaa virusi hivyo nchini Liberia. "

Amesema kama CAF inaendelea kuwahamisha wadau wote wa mchezo wa kandanda barani Afrika kuhusu namna ya kupambana na kitisho cha Ebola na kupunguza uwezekano wa kusambaa virusi hivyo."Tumeyandikia barua mashirikisho yote 54 ya CAF. Tumewapa vidokezo kuhusu namna ya kupata maelezo zaidi kuhusu Ebola, ili nayo yawavifahamishe vilabu vyao, kwa sababu siyo timu tu za kitaifa Afrika ambazo zitasafiri Septemba. Kuna mechi za Ligi ya Mabingwa kwa vilabu na Kombe la Mashirikisho. Kwa hivyo inahusu vitengo vyote vya soka la Afrika".

Mwandishi: Bruce Amani/AFP
Mhariri: Yusuf Saumu