1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Cameron ahusishwa na Panama

Admin.WagnerD8 Aprili 2016

Dhoruba ya kashfa ya kile kinachoitwa "Panama Papers" inaendelea kufukuta, Waziri Mkuu wa Uingereza David Cameron amekiri kunufaika na kampuni ya baba yake iliyosajiliwa nchini Panama.

https://p.dw.com/p/1IRsR
Großbritannien Premierminister David Cameron
Waziri Mkuu wa Uingereza David CameronPicha: Reuters/F. Lenoir

Waendesha mashitaka nchini Argentina wamefungua kesi dhidi ya rais wa taifa hilo Mauricio Marcri.

Viongozi kadhaa wa mataifa, watu maarufu na wanamichezo maarufu wamehusishwa na tuhumua zilizo katika uchunguzi wa vyombo vya habari za nyaraka milioni 11.5 zilizovuja kutoka katika kampuni ya Kipanama inaoyotoa ushauri wa kisheria ya Mossac Fonseca.

Cameron ambae amekuwa akijihami juu ya kubainika kwa mipango ya kifedha ya kisiri ya matajiri na watu wenye ushawishi, amekiri kuwa na hisa zenye thamani ya paundi 30,000 katika kampuni hiyo ambayo uwekezaji wake ulianzishwa na baba yake.

Akizungumza na kituo cha televisheni cha ITV cha Uingereza waziri mkuu huyo alisema aliuza hisa katika kampuni yenye makao yake makuu huko Bahamas mnamo mwaka 2010, ikiwa miezi minne kabla ya kuchukuwa wadhifa wa waziri mkuu wa Uingereza. Lakini waziri mkuu huyo wa Uingereza alisisitiza kuwa alilipa kodi ya mapato kutokana na mgao wa mauzo ya hisa hizo, alizonunua mwaka 1997.

Rais wa Argenitina matatani

Kashfa ya Panama imemwangusha waziri mkuu wa Iceland na kulazimisha wanasiasa wengine wakubwa kuingia katika hatua kali za kujihami akiwemo rais wa Urusi Vladimir Putin, rais wa China Xi Jinping na sasa rais Macri wa Argentina, kiongozi wa mrengo wa kulia anaechipukia katika eneo la Amerika ya Kusini.

Mauricio Macri Präsident Argentinien beim Nuklear-Gipfel in Washington
Rais wa Argentina Mauricio MacriPicha: Getty Images/R. Sachs-Pool

Lakini kiongozi huyo amesisitiza hakwenda kinyume na mamlaka yake ya kumiliki mali za umma kama afisa wa serikali, baada ya mwendesha mashitaka mkuu wa serikali Federico Degado kumuomba jaji aombe taarifa za mamlaka ya mapato ya taifa na ofisi ya kukabiliana na rushwa ili kuweza kuchunguza kama kuna uwezekano wa rais huyo kufanya kosa la uhalifu wa kifedha.

Rais huyo wa kihafidhini ni miongoni mwa walitajwa katika bodi ya wakurugenzi wa makampuni mawili, moja likiwa limesajiliwa Bahamas na lingine Panama. Hakutanagaza mali anazomiliki pale alipochaguliwa kuwa Meya wa Buenos Aores mwaka 2007 au kuwa rais Desemba mwaka jana.

Mwandishi: Sudi Mnette/AFP
Mhariri: Iddi Ssessanga