1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

CANCUN:Kimbunga Dean chapungua kasi

21 Agosti 2007
https://p.dw.com/p/CBX3

Kimbunga Dean ambacho kimelikumba eneo la pwani ya Mexico, kimepungua nguvu yake mnamo wakati ambapo kinaelekea katika eneo la nchi kavu.

Kimbunga hicho kiliipiga pwani hiyo mapema leo kikiwa katika daraja la tano la nguvu za vimbunga, huku kasi ya upepo wake ikiwa ni kilomita 260 kwa saa.

Lakini kwa mujibu taarifa za kituo cha hali ya hewa cha Marekani kasi hiyo hivi sasa imepungua na kuwa kilomita 205 kwa saa na kupungua nguvu kutoka daraja la tano hadi la tatu la vibunga.

Kimbunga hicho kimeelekea maeneo ya kaskazini mashariki mwa Mexico na tayari kimeupiga mji wa Chetumal na kwa mujibu wa watalaam kimbunga hicho kinatarajiwa kupiga katika maeneo ya nchi kavu huko mexico keshokutwa.

Tayari watu 12 wamekwishakufa toka kimbunga hicho kinachoambatana na mvua kubwa kilipopiga katika maeneo ya Haiti, Jamuhuri ya Domonica, Santa Lucia, Martinique, Dominica na Jamaica.

Maelfu ya watalii wameondoka kutoka katika maeneo ya pwani ya Mayan Riviera nchini Mexico, wakihofu kimbunga hicho ambacho pia kinatishia visima vya mafuta vilivyoko katika eneo hilo.