1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

CARACAS: Rais Chavez ataka kukutana na waasi wa Kimaksi

16 Septemba 2007
https://p.dw.com/p/CBPU

Rais Hugo Chavez wa Venezuela amemtaka mwenzake wa Colombia, Alvaro Uribe, amruhusu akutane na kiongozi wa kundi la waasi la Kimaksi la FARC kujadili kubadilishana mateka.

Rais Chavez pia amependekeza kwamba rais wa Ufaransa, Nicolas Sarkozy, anaweza kushiriki kwenye mazungumzo hayo. Miongoni mwa mateka wanaozuiliwa na kundi la FARC ni mwanasiasa mwenye uraia wa Ufaransa na Colombia, Ingrid Betancourt.

Rais Chavez amependekeza pia rais Alvaro Uribe wa Colombia ahudhurie mazungumzo hayo.

Rais Hugo Chavez amejitwika jukumu la kuwa mpatanishi kati ya waasi wa Kimaksi na rais Uribe kwa kujaribu kuongoza mazungumzo yanayolenga kuwaokoa mateka 45 wanaozuiliwa na waasi hao.

Kundi la FARC linaitaka serikali ya Colombia iwaachie huru mamia ya waasi wa kundi hilo wanaozuiliwa katika magareza nchini humo.