1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Catalonia yatangaza uhuru, Uhispania yajiandaa kuichukuwa

Iddi Ssessanga
27 Oktoba 2017

Uhispania imekumbwa na matetemeko mawili ya kisiasa kwa wakati mmoja. Bunge la Catalonia limepiga kura kuanzisha mchakato wa uhuru, huku serikali kuu ya Uhispania ikipata mamlaka ya kulitawala moja kwa moja.

https://p.dw.com/p/2mdp4
Spanien Barcelona - Befürwörter der Unabhängigkeit vor Katalanischem Regionalparlament
Picha: Getty Images/Y. Herman

Bunge la Catalonia limepitisha azimio linalotaka uhuru wa jimbo hilo kutoka Uhispania siku ya Ijumaa, katika hatua ya kujibu uamuzi wa waziri mkuu Mariano Rajoy kutumia ibara ya 155 ya katiba, inayoiruhusu serikali kuu kuchukuwa usimamizi wa maeneo yanayoasi.

Muungano unaotawala jimboni Catalonia wa Junts Pel Si - Pamoja kwa Ndiyo - na washirika wake wa mrengo mkali wa kushoto wa chama cha CUP waliwasilisha muswada wa azimio unaosema: "Tunaanzisha Jamhuri ya Catalonia kama taifa huru lenye mamlaka ya kidemokrasia na sheria ya kijamii.

"Baada ya kila kitu kilichosemwa, sisi kama wawakilishi wa kidemokrasia wa watu wa Catalonia, na tukitekeleza haki ya kujiamulia mambo yetu na kwa mamlaka tulioipata kutoka kwa watu wa Catalonia, tunaingia katika hali ya sheria ya mpito na kuasisiwa kwa Jamhuri," alisema spika wa bunge la Catalonia Carme Forcade.

Spanien Krise in Katalonien- Carles Puigdemont singt katalanische Hymne
Kiongozi wa Catalonia Puigdemont akiimba wimbo wa taifa wa Catalonia ndani ya bunge baada ya kura juu ya uhuru mjini Barcelona, Ijumaa Oktoba 27,2017.Picha: picture-alliance/AP Photo/M. Fernandez

Tangazo hilo hata hivyo lilikuwa sehemu ya utangulizi tu na halikuwekwa kwenye kura.

Badala yake wabunge walitakiwa kupigia kura hatua zinazoelekea kwenye uhuru, kama vile kuiagiza serikali kuu ya Catalonia kuunda benki kuu, kuanzisha mchakato wa kuandika katiba na kutafuta utambuzi wa kimataifa.

Utata huo unalenga kumkinga rais wa Catalonia Carles Puigdemont na washirika wake dhidi ya hatari yoyote ya kukamatwa kwa uasi, kosa ambalo linabeba kifungo cha hadi miaka 30 gerezani.

Lakini mbinu ilionekana kutomsaidia Puigdemont baada ya mwendesha mashitaka wa serikali kufungua mashitaka y auasi dhidi yake, na mahakama ilitarajiwa kuamua iwapo ikubali mashitaka dhidi ya kiongozi huyo.

Rajoy aapa kuzuwia uhuru huo

Waziri Mkuu wa Uhispania Mariano Rajoy ametoa wito wa utulivu kufuatia kura hiyo mjini Barcelona. "Naomba utulivu kwa Wahispania wote," aliandika Rajoy kwenya ukurasa wake wa Twitter, na kuongeza kuwa, "utawala wa sheria utarejeshwa Catalonia.

Rajoy alisema awali kwamba hakukuwa na njia mbadala kwa ibara ya 155, ambayo chini ya vipengele vyake serikali mjini Madrid inataka kuifukuza serikali ya Puigdemont, kuchukuwa udhibiti wa vyombo vya habari vya umma na jeshi la polisi, na kuitisha uchaguzi wa jimbo ndani ya muda wa miezi sita.

Rajoy aliitisha kikao cha dharura cha baraza la mawaziri saa moja kwa saa za Afrika Mashariki, baada ya baraza ka seneti kupiga kura na kuipa mamlaka serikali yake ya kihafidhina kuweka utawala wa moja kwa moja jimboni Catalonia.

Spanien Krise in Katalonien- Mariano Rajoy
Waziri Mkuu wa Uhispania Mariano Rajoy akiwasili katika bunge le Seneti mjini Madrid Ijumaa Oktoba 27.10.2017 alikoomba idhini ya kulitawala jimbo la Catalonia baada ya kujitangazia uhuru.Picha: picture-alliance/AP Photo/P. White

Lakini rais wa Catalonia Puigdemont amewataka wafuasi wake kusimama kidete kwa njia ya amani, huku kundi la waliounga mkono azimio la uhuru katika bunge wakiwataka wakaazi wa jimbo hilo kutotii tena maagizo kutoka mjini Madrid.

Viongozi watangaza mshikamano na Uhispania

Rais wa Baraza la Ulaya Donald Tusk amesea serikali ya Madrid inaendela kuwa mshirika wa Umoja wa Ulaya na kuongeza kuwa laazima katiba iheshimiwe na hilo ni jambo lenye umuhimu wa kipekee kwa umoja huo.

Umoja wa Ulaya umesimama imara nyuma ya serikali ya Uhispania katika mgogoro huo ulioanza baada ya Catalonia kufanya kura ya maoni kuhusu uhuru.

Msemaji wa serikali ya Ujerumani Steffen Seibert, alisema Ujerumani haitotambua tangazo la upande mmoja la uhuru wa Catalonia, na kutoa wito wa majadiliano. Seibert alisema kupitia ukurasa wake wa Twitter kuwa uhuru na mipaka ya Uhispani hauwezi kuvunjwa.

Naye rais wa Ufanra Emmanuel Macron, alisema waziri mkuu Mariano Rajoy ana uungwaji mkono wa Ufaranda katika kurejesha utawala wa sheria jimboni Catalonia. Marekani, Uingereza pia zilisema bado zinaichukulia Catalonia kuwa sehemu ya Uhispania.

Mwandishi: Iddi Ssessanga/dpae,afpe,

Mhariri: Daniel Gakuba