1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Chama cha AfD chakumbwa na mgogoro wa ndani

Zainab Aziz
5 Oktoba 2017

Kiongozi wa chama cha AfD cha mrengo mkali wa kulia au maarufu kama chama mbadala kwa Ujerumani amesema hawezi kutabiri iwapo chama chake hakitakumbwa na kasoro za wanachama wake zaidi kuondoka kwenye chama hicho.

https://p.dw.com/p/2lHoi
Deutschland Alexander Gauland, Alice Weidel und Frauke Petry  in Berlin
Picha: Reuters/W. Rattay

Chama hicho cha mrengo mkali wa kulia cha nchini Ujerumani cha AfD kilipata zaidi ya asilimia 12.6 katika uchaguzi uliomalizika mwezi uliopita lakini chama hicho kinakabiliwa na malumbano ya ndani tangu wakati huo. Kiongozi wa chama hicho Alice Weidel ambaye pia ni kiongozi mwenza wa kundi la wabunge wa chama hicho sambamba na Alexander Gauland alizungumza katika mkutano wa chama hicho ulioandaliwa kwa ajili ya kuwachagua manaibu wapya watakao kiwakilisha chama hicho bungeni, Bibi Alice Weidel amesema anahofia labda huenda wanachama wengine wawili wakakitoka chama hicho maarufu kama chama mbadala kwa Ujerumani.

Hayo yanatokea siku moja tu tangu kutangaza kujitoa kutoka kwenye chama hicho mjumbe mpya aliyechaguliwa Mario Mieruch ambaye amesema amechukua hatua hiyo kutokana na msimamo mkali wa mrengo wa kulia unaochukuliwa na chama hicho cha AfD. Mwanachama mwingine aliyetoka ni Frauke Petry ambaye zamani ndiye aliyeonekana kama nembo ya chama hicho alitangaza kujiondoa kwake mara baada kumalizika uchaguzi mkuu wa nchini Ujerumani wa tarehe 24 mwezi Septemba. Petry ameshasema kuwa anatarajia kuunda chama kipya ambacho kitakuwa ni chama kitakacho wavutia wapiga kura wanaopendelea msimamo wa kihafidhina. Na kabla ya azma yake hiyo kutimia anahitaji kuwa na wabunge 35 kati ya jumla ya wabunge 95 waliochaguliwa ndipo atakapoweza kuunda kundi lake bungeni.  Mumewe pia alitoka kwenye chama hicho cha AfD.

Deutschland Pressekonferenz mit Dr. Frauke Petry
Aliyekuwa kiongozi wa AfD Frauke Petry Picha: picture-alliance/Eventpress

Je chama cha AfD kitadumu?

Wakati huo huo uchunguzi wa maoni uliofanywa na shirika la habari la DPA la nchini Ujerumani unaonyesha kuwa wengi kati ya wananchi wa Ujerumani wanaamini kuwa chama hicho cha AfD hakitadumu kwa muda mrefu katika uwakilishi wake katika bunge la Ujerumani - Bundestag. Asilimia 54 ya watu waliohojiwa wamesema wanaamini kwamba chama cha AfD ambacho hakipendelei wageni hakina nafasi ya kudumu bungeni hata hivyo ni asilimia 27 pekee ya wajerumani ndio wanaoamini kuwa chama hicho mbadala kwa Ujerumani kitafaulu kujizatiti na kuendelea kubakia bungeni kwa kipindi cha miaka minne ijayo. Kura hiyo ya maoni iliwahusisha takriban watu 2000.

Chama hicho cha AfD sio chama cha kwanza chenye kulemea mrengo mkali wa kulia kuwahi kutokea hapa nchini Ujerumani tangu kumalizika vita vya pili vya dunia ila kumewahi kuwepo vyama vyenye misimamo mikali ya kulia kama chama cha NDP chama cha Republicans na kile cha German People's Union na vyote hivyo vilipata umaarufu mkubwa kabla kutoweka ndani ya muda mfupi tu. hata hivyo wafuasi wa chama cha AfD wana matarajio makubwa kwa chama chao kilichoanzishwa mnamo mwaka 2013. 

Mwandishi: Zainab Aziz/DPAE

Mhariri: Iddi Ssesanga