1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Chama cha MDC nchini Zimbabwe kupiga kura iwapo kitashirikiana na rais Mugabe

Jane Nyingi/ AFPE..Picha AFP29 Januari 2009

Siku moja kabla ya upinzani nchini Zimbabwe kuamua iwapo utajiunga na serikali ya rais Robert Mugabe au la balozi wa Marekani nchini humo ameelezea matumani yake kuwa serikali ya umoja wa taifa itaundwa haraka.

https://p.dw.com/p/GjdZ
Morgan Tsvangirai,(kushoto) kiongozi wa chama cha MDC,Rais Robert Mugabe wa Zimbabwe(kulia)Picha: AP

James McGee amesema hayo wakati alipoitembelea zahanati zinazotoa matibabu kwa wagonjwa wa kipundupindu mjini Harare.Baada ya waziri wa zamani wa mashauri ya kigeni wa Marekani bi Condolezza Rice kusema mwaka jana kwamba rais Mugabe anapaswa kuachia madaraka,Marekani sasa inaonekana kuridhia hatua ya rais Mugabe kuongoza serikali ya muungano wa kiataifa.

Kwa mujibu wa makubaliano ya September mwaka jana, Mugabe atabakia rais na Morgan Tsvangirai kuchukua nafasi ya waziri mkuu katika serikali itakayokijumuisha chama tawala cha ZANU-PF na cha upinzani MDC.

Baada ya miezi minne ya kusubiri iwapo kutafikiwa makubaliano yatakayouridhisha upinzani kuhusu kugawana madaraka na chama cha rais Mugabe,chama cha MDC kinatarajiwa kupiga kura kesho ijumaa iwapo kitashirikiana na rais Mugabe au la.


Kiongozi wa chama cha MDC Tsvangirai amekubaliana na hatua hiyo akisubiri kutatuliwa kwa baadhi ya maswala. Matamshi hayo ya balozi wa Marekani nchini Zimbabwe yanawadia huku mashirika ya kutoa misaada nchini humo yakitangaza hali ya hatari kutokana na uhaba wa chakula.Karibu wazimbabwe millioni 11 ambao ni nusu ya idadi ya watu nchi hiyo wanahitaji msaada wa chakula.


Wito wa misaada kwa Wazimbabwe kutoka mashirika kama shirika la chakula duniani,Oxfam na mengineyo yasiyoya kiserikali yalioko nchini humo umekua ukipuuzwa na mataifa ya magharibi.


Hali hiyo imeathiri huduma za matibabu kwa waliokumbwa na ugonjwa wa kipundupindu,huku idadi ya waliofariki tangu kuzuka kwa ugonjwa huo Agosti mwaka jana ikifikia watu elfu tatu.Ugonjwa huo umesambaa kwa haraka kutokana na kuvurungika kwa miundo msingi.