1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Champions League-kombe la ulaya

19 Februari 2008

kombe la klabu bingwa barani Ulaya larudi uwanjani leo huku Real Madrid ikijiwinda kutamba nyumbani mwa AS Roma.

https://p.dw.com/p/D9vd

Kombe la klabu bingwa barani ulaya linarudi uwanjani leo baada ya likizo ya x-masi na mwaka mpya huku mabingwa mara 9 Real Madrid ya Spain ikiwa imevinjari leo kuimaliza AS roma ya Itali nyumbani mwao Roma.

Viongozi wa Ligi ya Itali (Serie A) Inter Milan wana miadi leo na Liverpool ya uingereza mjini Liverpool.Chelsea ikitiwa moyo na kurudi uwanjani kwa Frank Lampard na nahodha wao John Terry wanapambana na Olympiakos Piraeus ya Ugiriki mjini Athens wakati waakilishi wa Ujerumani Schalke 04 wanawakaribisha nyumbani Gelsenkirchen FC Porto ya ureno.

Ikicheza nyumbani Schalke lazima itambe leo ikiwa inataka kweli kubakia hayi katika changamoto za champions League na kuendelea kupepea bendera ya Ujerumani wakati m,abingwa Bayern Munich wanatamba katika kombe la ulaya la UEFA.

Liverpool inaingia uwanjani leo baada ya kuzabwa mabao 2-1 mwishoni mwa wiki na timu ya daraja ya pili Barnsley katika kombe la FA.Kocha wa Liverpool Rafa Benitez ambae klabu yake hii iko nafasi ya 5 ya ngazi ya ligi ya Uingereza anaelewa vyema kwamba pigo jengine leo ni buriani kwa muda mrefu katika champions League.

Inter Milan inayopania kuivua taji AC Milan mahasimu wao wa mtaani huko Itali, iliwapumzisha kucheza mastadi wake 2 –Zlatan Ibrahimovic na Julio Cruz mwishoni mwa wiki lakini, wote wanarudi lleo uwanjani kwa changamoto hii ya kwanza na Liverpool tangu 1965.

Chelsea imeimarishwa na kurudi uwanjani kwa Frank Lampard na nahodha wao john Terry na wana kila matumaini ya kutamba mbele ya wagiriki Olympiakos.

Mabingwa watetezi wa kombe hili la ulaya AC Milan wana mlima mrefu kuupanda kesho watakapokutana na Arsenal London.Hivyo ndivyo aonavyo Fabio Capello-kocha wa sasa wa Uingereza, alieiongoza AC Milan kutamba kwa mabao 4-0 dhidi ya Barcelona katika finali ya 1994.

Manchester united ambayo capello anaamini ndio majogoo watakaowika msimu huu na kutwaa kombe hili la Ulaya wana miadi na Lyon ya Ufaransa hapo kesho.

FC Barcelona ilioitimua Arsenal London kutwaa ubingwa wa 2006 wana miadi na Glagow Celtic wakati Sevilla mabingwa wa kombe la Ulaya la UEFA miaka 2 iliopita mfululizo wanafunga kesho safari ya Istanbul,Uturuki kutimiza miadi yao na Fernerbahce. Barcelona imepunguza hofu na wasi wasi wake kidogo tangu kurejea kutoka kombe la Afrika kwa samba wa nyika Samuel Eto’o .Eto alikosa kucheza katika mpambano na Real zaragosa jumamosi ulioleta ushindi wa mabao 2-1 anapata nafuu sasa.

Kocha wake Frank Rijkaard sasa ana kikosi chake kamili kikijumuisha Eto’o mwenyewe, Lionel Messi wa Argentina,Ronaldinho wa Brazil na Thierry Henry wa Ufaransa.