1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

China na Marekani kutafuta mwanzo mpya?

7 Juni 2013

Rais Barack Obama na mwenzake wa China Xi Jinping kukutana katika mkutano wa aina yake,kusini mwa Carlifonia kujaribu kuunda uhusiano mzuri zaidi.

https://p.dw.com/p/18ldF
Barack Obama na Xi Jinping
Barack Obama na Xi JinpingPicha: Reuters

Rais Barack Obama wa Marekani na Xi Jinping wa China watakutana leo(Ijumaa)Tarehe 07.06.2013 katika mkutano wa aina yake kwenye eneo la kifahari la Sunnyland kusini mwa califonia,lengo likiwa ni kila upande kupata nafasi ya kufahamu malengo ya upande mwingine. Rais Barack Obama na mgeni wake Xi Jinping watakutana kwa siku mbili katika mazingira ya utulivu na faragha.

Mkutano huo unaoangaliwa kama nafasi muhimu kwa pande zote mbili kujuwana zaidi nia na malengo ya kila upande kuhusu masuala mbali mbali.Nchi zote mbili zina nguvu za kiuchumi,ni nchi za kubwa kibiashara na zote mbili ni wachafuzi wakubwa wa mazingira duniani.

Barack Obama na aliyekuwa rais wa China Hu Jintao
Barack Obama na aliyekuwa rais wa China Hu JintaoPicha: JEWEL SAMAD/AFP/Getty Images

Kwa upande mwingine Marekani ni mdaiwa mkubwa duniani na china ni mfadhili mkubwa wa nchi za kigeni.Kwa maana hiyo yapo mengi yakujadiliwa kati ya viongozi hao wawili kuhusu masuala ya kiuchumi.Ni ziara ya kwanza nchini Marekani kwa Xi Jinping akiwa kama rais wa China miezi kadhaa baada ya kuchukuwa uongozi wa dola la China na kwahivyo wadadisi wanaofuatilia kwa karibu siasa za China na Marekani wanaona mkutano huo adimu kama jukwaa muhimu kabisa kati ya pande hizo mbili kwa kipindi cha miaka mingi.

Hali ya Kutoaminiana

Rais Obama atapata nafasi ya kutafuta maingiliano mazuri zaidi ya kisiasa ambayo yanaweza kumuongezea sifa katika kipindi chake madarakani hasa kutokana na wakati mgumu ulioshuhudiwa huko nyuma,chini ya rais Hu Jintao.

Kimsingi viongozi hao wawili hawakupangiwa kukutana haraka hivi bali ilitegemewa wangekutana katika mkutano wa kilele wa nchi za kundi la G20 huko Urussi mwezi wa Septemba lakini inavyoonyesha kila upande unahisi pana umuhimu na haja ya kukutana hasa kufuatia kuonegezeka wasiwasi na hali ya kutoaminiana ambazo zinaongeza kuleta hali ya mkanganyiko na kuuharibu uhusiano.

Tayari ikulu ya Marekani inabashiri kwamba hakuna maafikiano yoyote yatakayotokana na mkutano huo,sababu zinatokana kwanza na ratiba iliyopo na jingine ni kwamba masuala yanayowakabili viongozi wote wawili ni tete mno.Juu ya hilo inategemewa kwamba patakuwa na mazungumzo marefu ya majibizano juu ya suala ya usalama wa mitandao kufuatia msururu wa visa vinavyotaja kwamba China imeiba siri nyingi za kijeshi na kibishara za Marekani. China imeshaashiria kwamba hata nayo imekuwa muhanga wa hujuma hizo na itakuwa tayari kujitetea dhidi ya shutuma za Marekani.

Rais wa zamani wa Marekani George W. Bush na rais wa zamani wa China Hu Jintao
Rais wa zamani wa Marekani George W. Bush na rais wa zamani wa China Hu JintaoPicha: ANATOLY MALTSEV/AFP/Getty Images

Obama na Jinping wanatazamiwa kukutana usiku kabla ya mazungumzo rasmi na baadae kujumuika pamoja kwa chakula na kisha kukutana tena Jumamosi asubuhi.

Mwandishi:Von Hein Matthias/Yusuf Saumu/afpe

Mhariri:Mohammed AbdulRahman