1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Clinton nchini Pakistan

21 Oktoba 2011

Waziri wa mambo ya nchi za kigeni wa Marekani Bi Hillary Clinton, ameonya hatua kali zinafaa kuchukuliwa dhidi ya vikosi vya Afghanistan na Pakistan iwapo havitashirikiana kuweka amani Afghanistan.

https://p.dw.com/p/12wi8
Waziri wa mambo ya nchi za kigeni Bi Hillary ClintonPicha: AP

Waziri huyo wa mambo ya nchi za Kigeni bi Hillary Clinton amesema baada ya miaka kumi ya mapigano, sasa imefikia wakati wa kuwakamata waasi wa kundi la Taliban walioko Afghanistan na Pakistan pamoja na kundi linaloshukiwa kushirikiana na kundi la al Qaeda, Haqqani.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Islamabad Clinton amesema ni lazima makundi ya waasi wa taliban nchini Pakistan na Afghanistan, kundi la waasi la Haqqani pamoja makundi yote ya kigaidi yaletwe pamoja katika makubaliano ya kudumisha amani katika nchi hizo. Clinton ameongezea kuwa iwapo hilo halitawezekana; basi ni lazima kutafutwe njia muafaka za kuzuia makundi haya kusababisha maafa zaidi ya watu wasio na hatia.

Msukumo wa Islamabad kuchukua harakati muhimu dhidi ya waasi umezidi, tangu vikosi maalum vya Marekani vilipomkamata na kumuua kiongozi mkuu wa kundi la kigaidi la Al Qaeeda Osama Bin Laden mwezi Mei mwaka huu, katika mji mmoja nchini Pakistan ambapo kiongozi huyo alikuwa akijificha kwa miaka mingi.

USA Afghanistan General David Petraeus in Washington
Mkurugenzi wa shirika la kijasusi nchini Marekani CIA, Generali David PetraeusPicha: dapd

Hapo jana Bi Clinton, pamoja na mkurugenzi wa shirika la kijasusi la marekani CIA David Petraeus na mwenyekiti wa viongozi wakuu wa jeshi generali Martin Dempsey, walitoa ujumbe mkali kwa viongozi wa pakistan kuwasaka waasi haswa wa kundi la taliban na Haqqani kutokana na shutuma za mashambulizi ya Marekani nchini Afghanistan.

Kusakwa kisiri kwa Osama Bin Laden na vikosi maalum vya Marekani kulisababisha hali ya wasiwasi kati ya Marekani na Pakistan ambao walijiunga na kikosi cha kupambana na ugaidi baada ya shambulio la september 11 nchini marekani.

Hata hivyo Pakistan inasema msako huo uliofanywa na Marekani unadhalilisha haki na uhuru wa nchi hiyo, huku maafisa wakuu wa Marekani wakijiuliza iwapo Pakistan ilikuwa inamficha kiongozi huyo wa kigaidi Osama Bin laden, kwa upande wao Pakistan wanasema hawakuwa na habari yoyote kama Osama alijificha huko.

Hata hivyo katika ziara yake ya siku mbili nchini pakistan, Bi Hillary Clinton akizungumza karibu na mwenzake wa pakistan Hina Rabbani Khar, amehimiza serikali ya nchi hiyo kuweka nguvu zake katika kuwakamata makundi ya kigaidi haswa la Haqqani linaloaminika kujificha katika maeneo ya kaskazini mwa Waziristan karibu sana na mpaka wa Afghan.

Muandishi Amina Abubakar/RTRE

Mhariri Yusuf Saumu