1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Clinton barani Afrika.

Abdu Said Mtullya12 Agosti 2009
https://p.dw.com/p/J8Yj
Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Hillary Clinton.Picha: picture alliance / landov

Waziri wa mambo ya  nje  wa  Marekani Hillary Clinton ameitaka Nigeria iwe na msimamo thabiti  katika  kupambana na rushwa na  ameahidi msaada ili  kuunga mkono juhudi za kuleta mageuzi katika mfumo wa uchaguzi.

Akizungumza  kwenye mkutano  na waandishi habari pamoja  na  waziri  wa mambo ya nje  wa Nigeria ,waziri Clinton amesema leo mjini Abuja  kuwa nchi   yake inaunga  mkono thabiti juhudi za   serikali ya Nigeria  za kuleta uwazi zaidi,   na kupunguza rushwa .

Waziri Clinton pia amesema kuwa Marekani ipo tayari kusaidia katika  kuanzisha michakato ya demokrasia   ikiwa ni sehemu ya  matayarisho ya  uchaguzi utakaofanyika mwaka 2011.

Rushwa  pamoja na usimamizi mbaya   wa raslimali vimekwamisha  maendeleo,   vitega uchumi ,vimehujumu demokrasia na kusababisha migogoro katika jimbo  la  Niger Delta na mvutano wa kidini  kaskazini mwa Nigeria.

Akijibu kauli  ya waziri Clinton  ,waziri  wa mambo  ya nje  wa Nigeria bwana Ojo Maduekwe amesema kuwa, nchi yake inatambua kwamba kukosolewa  hakuna maana  ya kukasirishwa  ama kuchochea mabaya.

Waziri Maduekwe pia amesema  anatambua kwamba wanaoikosoa Nigeria wanaitakia mema. Hatahivyo amesema serikali ya Nigeria imezingatia wasiwasi na  yaliyosemwa na rafiki.

Katika ziara yake ya nchi kadhaa barani Afrika  waziri wa mambo ya nje wa Marekani Clinton amekuwa  anasisitiza ujumbe juu ya kupambana na  rushwa Katika  ziara  yake nchini Nigeria waziri  wa mambo ya nje wa Marekani Hillary   Clinton pia atakutana na rais Umaru Yar'Adua. Kesho ataelekea Liberia.