1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

CONAKRY : Rais Conte aomba kurefusha sheria ya kijeshi

23 Februari 2007
https://p.dw.com/p/CCPc

Rais Lansane Conte wa Guinea hapo jana amelitaka bunge kuidhinisha kuongeza muda wa sheria ya kijeshi iliowekwa nchini kote siku 10 zilizopita kuzima ghasia za matumizi ya nguvu dhidi ya serikali.

Spika wa bunge la taifa Aboubakar Sompare ameiambia televisheni ya taifa kwamba wamepokea ombi kutoka kwa rais la kurefushwa kwa sheria ya kijeshi ombi ambalo watalitafakari leo hii.

Katiba ya Guinea inahitaji bunge kuidhinisha kuongezwa muda kwa sheria ya kijeshi ambao awali iliamuriwa imalizike hapo Februari 23 kukabiliana na mgomo wa kitaifa na maandamano ya upinzani nchini kote dhidi ya Conte.

Viongozi wa mgomo huo wa kazi wanadai Konte akiwa na umri wa miaka ya sabini na kitu an’gatuke madarakani baada ya kuitawala nchi hiyo kwa miaka 23.Walianzisha tena mgomo huo baada ya rais huyo kumchaguwa rafiki yake wa karibu Eugene Camara kuwa waziri mkuu licha ya kukubaliana kwamba atamchaguwa mtu watakemuafiki.

Zaidi ya watu 120 takriban wote wakiwa ni raia wameuwawa kuanzia mwanzoni mwa mwaka huu katika mapambano kati ya vikosi vya usalama vya serikali na waandamanaji.