1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Daimler latengana na Chrysler

Oummilkheir15 Mei 2007

Ilikua hasara tupu wanasema wahariri wa magazeti ya Ujerumani

https://p.dw.com/p/CHSx

Makampuni ya magari ya DAIMLER na CHRYSLER yametengana baada ya miaka tisaa ya pamoja.Kampuni la DaimlerChrysler lenye makao yake makuu mjini Stuttgart limeliuzia shirika la uwekezaji tawi lake la kimarekani.Wahariri takriban wote wa magazeti ya Ujerumani wameshusha pumzi baada ya jinamizi kutoweka.

Gazeti la NORDBAYERISCHE KURIER la mjini BAYREUTH linaandika:

„Hatimae wameachana- watu ambao kamwe hawajawahi kulingana:Baada ya miaka tisaa ya kuishi pamoja,ndowa ya Daimler na Chrysler imevunjika.Kutengana nkwao kumezusha wimbi la furaha na vigelegele katika soko la hisa.Si ajabu.Makosa ya JURGEN SCHREMP yamesawazishwa na Dieter ZETSCHE.Kampuni la Damler AG litaweza siku za mbele kujishughulisha na kile inachokiweza zaidi:yaani kutengeneza magari ya fakhari na ya ghali yanayotia faida.Shughuli zinazotia hasara za kutengeneza magari chungu nzima kandoni mwa magari ya anasa,zimeachiliwa mbali na ZETSCHE.“

Hata gazeti la SÜDDEUTSCHE ZEITUNG linahisi ZETSCHE amerekebisha makosa yaliyofanywa na mtangulizi wake Schremp.Gazeti linaendelea kuandika:

„Schremp alifikiri hakuna mjuzi kama yeye,aliamini angeweza kulidhibiti soko lote.Kimsingi lakini alikua akiendesha shughuli zake bila ya kuwatilia maanani wafanyakazi,wateja wala wenye hisa na kusababisha hasara ya mabilioni ya yuro.Yule ambae wakati mmoja alisifiwa kama kiongozi bora kuliko wote ameshindwa vibaya sana kama uwanja wa kiuchumi.Mtu hatokosea akisema kwamba kasheshe ya Damler chanzo chake ni Schremp-angalao kwa sehemu.“

Gazeti la mjini Bonn, GENERAL ANZEIGER linachambua:

„Kwa kuliuza kampuni la CHRYSLER,DAIMLER CHRYSLER limetaka kuufunga ukurasa wa historia ya kampuni lake ambao tokea mwanzo haukuwa na baraka.Hata hivyo hawakuachana moja kwa moja kwasababu Stuttgart inataka kuendelea kumiliki asili mia tano ya hisa za kampuni hilo la Marekani.Kujitenganisha kwa hivyo sio tuu inamaanisha mwisho wa ndowa kati ya makampuni ya magari,bali pia mwisho wa ndoto ya kuundwa shirika kubwa kabisa ulimwenguni-ambalo wamiliki hisa wa Stuttgart miaka nenda miaka rudi walikua wakilitegemea na kuwagharimu fedha chungu nzima.Muhimu kwa sasa ni makadirio.Na yanaonyesha yatakua mazuri sana kwa kampuni jipya la Daimler AG bila ya wamarekani.“

Gazeti la TAGESSPIEGEL la mjini Berlin linajiuliza:

„Jee zoezi lililoshindwa la DAIMLERCHRYSLER linaweza kuangaliwa kama ahadi tupu za utandawazi?Kuuziwa CERBERUS kampuni la Chrysler kunadhihirisha kinyume chake.Pekee mile hali kwamba shirika la uwekezaji ndilo lililofanikiwa kulinunua kampuni la Chrysler lililowekeza yuro bilioni 17.4 katika mashirika 50 yenye jumla ya wafanyakazi laki moja na 75 elfu,inadhihirisha maguvu na ushawishi walio nao kutokana na mtaji wao.Shirika la Private-Equity na HEDGE-FONDS ndio wana utandawazi wa kweli.Haimaanishi lakini kama wao ni wafanyabiashara wa kweli pia.Mtaji wao unaingia na kutoka,sawa na kuvutiwa kwao na shirika fulani,bidhaa na soko.Kama utaratibu huo utaleta tija pia katika viwanda vya magari-tusubiri tuone.