1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

DRC:Wanajeshi hatarini kuhukumiwa kifo kwa tuhuma za "woga"

30 Machi 2024

Waendesha mashtaka nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo wameitolea wito mahakama ya kijeshi mashariki mwa nchi hiyo, kutoa hukumu ya kifo kwa askari 11 wanaotuhumiwa kwa makosa ya "woga" na "kumkimbia adui".

https://p.dw.com/p/4eGVI
Wanajeshi wa serikali ya DRC-  FARDC
Wanajeshi wa serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo FARDCPicha: Dai Kurokawa/dpa/picture alliance

Askari hao walikuwa kwenye kituo cha Lushangi-Cafe, karibu na mji wa kimkakati wa Sake, takriban kilomita 20 kutoka Goma. Alexis Olenga, wakili wa Luteni Kanali Gabriel Paluku Dunia, mmoja wa maafisa watano wanaokabiliwa na mashtaka hayo, amekanusha tuhuma hizo na kusema kesi hiyo imeahirishwa hadi Aprili 5.

Soma pia: Tshisekedi azidi kutema cheche dhidi ya Rwanda, M23 washambulia tena Sake

Wito huu wa kutekelezwa adhabu ya kifo ni wa kwanza kutolewa tangu serikali mjini Kinshasa ilipoamua mnamo Machi 13 kurejesha hukumu ya kifo katika wakati ambapo waasi wa M23 wanaendelea kujiimarisha karibu na mji mkuu wa mkoa wa Kivu Kaskazini wa Goma. Mashirika ya kutetea haki za binadamu pamoja na Kanisa Katoliki yameitaka serikali kuachana kabisa na adhabu ya kifo.