1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

DRESDEN : Chama cha Merkel chaanza mkutano

27 Novemba 2006
https://p.dw.com/p/CCp0

Mdahalo mkali wa kukata na shoka juu ya mwelekeo wa chama cha kihafidhina cha Kansela Angela Merkel CDU unatishia kuweka kiwingu kwenye mkutano wa chama hicho uliofunguliwa hapo jana mjini Dresden

Mwishoni mwa juma mawaziri wakuu wa mikoa wa chama cha CDU ambao wengine walionekana kama wanaweza kuchukuwa nafasi ya Merkel ya uwenyekiti wa chama walikuwa na mahojiano na magazeti wa kile kinachoonekana kama midahalo ya hadhara juu ya kinavyopaswa kuwa chama hicho cha mageuzi.

Ukiwa ni mwaka mmoja baada ya ushindi wa chupuchupu uliomlazimisha kuunda serikali ya mseto ya muungano mkuu na wapinzani wake wa chama cha Social Demokrat Merkel amekuwa katika mapambano ya kushinikiza mamlaka yake kwenye chama hicho pamoja na kukipa chama hicho mweleko ulio wazi.

Ingawa kuna matumaini makubwa sana ya Merkel kuchaguliwa tena kukiongoza chama hicho uchunguzi wa maoni umeonyesha umashuhuri wa chama hicho umeshuka sana kuwahi kushuhudiwa katika kipindi cha miaka sita.