1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Dunia yaadhimisha siku ya chakula

Admin.WagnerD16 Oktoba 2013

Leo 16.10.2013 ni siku ya chakula duniani. Na kwa ajili hiyo shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa, FAO limetoa mwito wa kuweka mkazo katika kuhakisha upatikanaji wa mahitaji ya chakula duniani kote.

https://p.dw.com/p/1A0ZD
Wafanyakazi wakipakua chakula kutoka kwenya gari nchini Sudan Kusini.
Wafanyakazi wakipakua chakula kutoka kwenya gari nchini Sudan Kusini.Picha: AP

Kila mwaka katika siku ya leo tarehe 16 mwezi wa oktoba Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Umoja wa Mataifa FAO linaidhmisha kuwa siku ya chakula duniani. Ni siku ambapo shirika hilo liliundwa mnamo mwaka wa 1945 baada ya kumalizika vita kuu vya pili. Lengo la maadhimisho ya leo ni kuweka mkazo juu ya kuimarisha juhudi za kupambana na adui njaa duniani.

Watoto wa Kisomali wakipatiwa chakula mjini Mogadishu. Somalia ni moja ya mataifa yanayokabiliwa na uhaba wa chakula duniani.
Watoto wa Kisomali wakipatiwa chakula mjini Mogadishu. Somalia ni moja ya mataifa yanayokabiliwa na uhaba wa chakula duniani.Picha: dapd

Ni siku ya kuhamasisha ufahamu wa masuala ya njaa na uhaba wa chakula duniani, yanayomgusa kila mwanadamu . Kauli mbiu ya mwaka huu inasema "kudumisha mfumo endelevu wa upatikanaji wa chakula na lishe." Akitoa ujumbe katika kuiadhimisha siku hii ya leo Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa, FAO Jose Graziano da Silva amesema binadamu wenye afya wanategemea uhakika wa kupatikana kwa chakula.

Baadhi walia njaa, wengine huvimbiwa
Naye afisa mwandamizi wa shirika la FAO Alexander Meyback amesisitiza juu ya umuhimu wa siku hii. "Leo ni siku ya kuhamisha ufahamu juu ya baa la njaa, uhaba wa chakula na ni hatua gani tunaweza kuzichukua .Wapo watu milioni mia nane na 42 wanaosibika na njaa duniani. Pia wapo watu bilioni mbili wasiopata chakula cha kutosha duniani achilia mbali wale wasiopata lishe bora."

Afisa huyo wa sera, Mayback amekumbusha kwamba wakati watu wengi hawana chakula cha kutosha duniani, wapo watu wengine wenye maradhi ya kuvimbiwa kutokana na shibe ya kupita kiasi. Bwana Meybeck ameeleza kuwa hali hiyo inaweza kusababisha kuongezeka kwa matumizi ya raslimali. Ongezeko hilo litayaathiri mazingira na kusababisha matumizi makubwa ya maji, ardhi na raslimali nyingine.

Chakula kikiwa kimetupwa mjini New York. Utafiti moja nchini Uingereza ulionyesha kuwa nusu ya chakula kinachozalishwa duniani huishia katika mapipa ya taka.
Chakula kikiwa kimetupwa mjini New York. Utafiti moja nchini Uingereza ulionyesha kuwa nusu ya chakula kinachozalishwa duniani huishia katika mapipa ya taka.Picha: Getty Images

Malengo yanahitajika
Katika madhimisho ya siku ya leo duniani kote, Shirika la FAO linatoa mwito wa kwa kila mtu wa kufikiria juu ya kutafuta njia na kuweka malengo ya kipaumbele katika kuhakikisha upatikanaji wa chakula duniani. Shirika la FAO pia limetahadharisha juu ya ugeu geu wa bei za vyakula duniani.

Shirika la FAO limesema hali hiyo huenda ikaendelea kuisakama dunia kwa muda mrefu. Murugenzi mkuu wa shirika la FAO Jose Graziano da Silva amesema bei zitaendelea kugeuka geuka. Hata hivyo Mkurugenzi huyo amesema ughali umepungua kulinganisha na hali ya mwaka uliopita kutokana na ongezeko la uzalishaji wa nafaka.

Mkurugenzi huyo amezitaka nchi wanachama waitumie fursa ili kujitayarisha na hivyo kuweza kuikabili hali ya ugeu ugeu wa bei za vyakula kwenye soko la dunia.

Mwandishi.Mtullya Abdu/FAO
Mhariri: Mohamed Abdul-Rahman.