1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ehud Barak avunja ziara ya Ujerumani

C.Verenkotte/P.Martin4 Aprili 2008

Ziara ya Kansela Merkel wa Ujerumani hivi karibuni nchini Israel iliimarisha uhusiano kati ya nchi hizo mbili.Sasa lakini,Waziri wa Ulinzi wa Israel amesema hatofanya ziara yake ya Ujerumani,iliyopangwa hapo awali.

https://p.dw.com/p/Dbs2
Israeli Defense Minister Ehud Barak, right, stands with Israeli military chief Lt. Gen. Gabi Ashkenazi, during a welcoming ceremony at the Israeli Defense Ministry in Tel Aviv, Israel, Monday, March 31, 2008. Israel has approved the construction of almost 1,700 homes in contested territory since renewing peace talks with the Palestinians at a U.S.-hosted summit in November, an Israeli watchdog group reported Monday. (AP Photo/Nir Kafri, Pool)***Zu Verenkotte, Barak sagt Deutschland-Besuch ab - Spannungen zwischen Israel und Syrien***
Waziri wa Ulinzi wa Israel,Ehud Barak(kulia) pamoja na mkuu wa majeshi ya Israel Lt.Jenerali Gabi Ashkenazi mjini Tel AvivPicha: AP

Je,kuna uhusiano wo wote kati ya kuvunjwa kwa ziara hiyo na kuimarishwa kwa vikosi vya Syria mpakani na Israel?

Israel haina nia ya kuishambulia Syria.Hayo alitamka Naibu Waziri Mkuu wa Israel Haim Ramon kujibu ripoti za vyombo vya habari zilizosema kumezuka hali mpya ya mvutano kwenye mpaka wa Israel na Syria.Katika kurasa za mbele,magazeti mashuhuri ya Israel yamedai kuwa majeshi ya nchi hiyo yamewekwa katika hali ya tahadhari baada ya Syria kuimarisha vikosi vyake karibu na mpaka wa Israel.Jerusalem Post limesema hali ya mvutano iliyozuka mpakani na katika Ukanda wa Gaza ni mambo yaliyomfanya Waziri wa Ulinzi Ehud Barak kuifuta ziara yake nchini Ujerumani.

Lakini kwa mujibu wa msemaji wa serikali,uamuzi wa kuivunja ziara ya Ujerumani,unahusika na mazoezi ya kijeshi yaliyopangwa kufanywa juma lijalo pamoja na kujitayarisha kwa uwezekano wa kupambana na wanamgambo wa Hezbollah iwapo watajaribu kulipiza kisasi mauaji ya kiongozi wao wa kijeshi Imad Mughnieh. Wahezbollah wanailaumu Israel kuhusika na mauaji ya ya kiongozi wao wa kijeshi.Lakini Israel imekanusha kabisa madai hayo.Mugnieh aliuawa Februari 12 katika mripuko wa bomu la gari katika mji mkuu wa Syria,Damascus.

Alkhamisi mchana,duru za serikali ya Israel zilisema Hezbollah na Syria zilikuwa zikiwasiliana saa zote. Inasemekana kuwa 40 ya kiongozi wa kijeshi alieuawa imemalizika mwisho wa juma lililopita kwa hivyo wanamgambo wa Hezbollah wapo tayari kufanya mashambulizi yao.Hata hivyo,Jerusalem inaamini kuwa wanamgambo hao hawatoweza kushambulia bila ya hapo kabla kupata idhini ya Syria.Magazeti ya Israel yakadiria kuwa Syria imepata fununu za mpango wa Hezbollah na hivyo inajaribu kujiandaa kwa jawabu la kijeshi kutoka Israel.Lakini Naibu Waziri Mkuu wa Israel Ramon amesema: "Israel haina nia ya kuishambulia Syria.Ripoti zilizogonga vichwa vya habari hazina msingi wo wote.Nasema dhahiri kuwa Israel haina azma ya kuishambulia Syria."

Gazeti la kiarabu Al Quda al-Arabi linalochapishwa London, liliripoti kuwa Syria imepeleka vikosi vitatu vya vifaru na majeshi zaidi ya nchi kavu kwenye eneo la mpakani.Lakini,Naibu Jenerali wa majeshi ya Israel,Dan Harel amesema,yeye haoni sababu ya kuwepo mvutano katika eneo la kaskazini na vile vile anaamini kuwa hakuna anaetaka kujiingiza katika mapambano ya kijeshi.