1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Eintracht Braunschweig Mabingwa 1967

Ramadhan Ali6 Juni 2007

E.Braunschweig ilitamba 1967 ilipotawazwa mabingwa wa bundesliga.Msimu uliopita wakicheza daraja ya pili.

https://p.dw.com/p/CHc1

Tukiendelea na mlolongo wetu wa kuwajulisha klabu mashuhuri za Bundesliga-Ligi ya Ujerumani iliomalizika wiki 2 nyuma kwa kuitawaza VFB Stuttgart mabingwa wapya,leo ni zamu ya mabingwa wa zamani Eintracht Braunschweig.Klabu hii ilioasisiwa Dezemba 15,1895, inacheza daraja ya pili na haitambi tena hata huko kama miaka ya kati ya 1960ini.

Wimbo huo wa klabu ya Braunschweig haukuwahi kuhanikiza sana wala kusikika kwa urefu kama mwaka 1967-mwaka samba wa Braunschweig waliponguruma kweli na kutoroka na taji la ubingwa wa Ujerumani.

Mashabiki wa Eintracht Braunschweig tangu kuasisiwa kwa klabu hii hadi leo wamekuwa wakijionea klabu yao ikipanda na kushuka.

Baada ya Braunschweig kuibuka mabingwa wa Ujerumani ya kaskazini mara 2,mkondo ukiongoza chini.Timu hii ilianza kudhofika pale baragumu la vita vya pili vya dunia na 1945 Braunschweig ikatoweka.

Braunschweig ikafufuliwa tena kwanza kwa jina jengine kabisa-TSV kabla baadae hapo 1963 kurejea jina la asilia la Eintracht Braunschweig katika Ligi mpya nay a sasa Bundesliga.

Katika uwanja wake mpya unaochukua jumla ya mashabiki 38,000,timu hii chini ya usukani wa nahodha na kipa wake Hans Jäcker,iligeuka kikosi imara.

Hans Jocker anakumbusha:

“Hatukutetereka kabisa wala kuwa shaka shaka.Hatukupotewa na akili na usoni kabisa tukicheza kwa nguvu moja ari moja.”

Moyo na ari hiyo ikaiongoza Braunschweig kuzusha msisimko na maajabu 1967,kwani mwaka huo sio Bayern Munich iliopigiwa upatu na kuhanikiza ingetwaa taji,wala si Borussia Dortmund au Munich 1860 bali nahodha Jäcker na timu yake ndio iliotwaa ubingwa. Kocha wao wakati ule aliitwa Helmut Johannsen.Shangwe za ushindi zilikuwa kubwa mno.Halafu katika kinyan’ganyiro cha finali ya kombe la klabu bingwa barani Ulaya ikiwakilisha Ujerumani,Braunschweig haikusalim amri kirahisi ilipokumbana na Juventus turin ya Itali.

Lakini aliejuu mgonje chini.Baada ya mafanikio hayo msimu wa 1970-71 Eintracht Braunschweig ikakumbwa na kashfa iliozuka katika Bundesliga na hilo likawa kaburi lake la kuizika.Waliohusika hasa walikuwa viongozi wa klabu 2-Kickers Offenbach na Armenia Bielefeld ambazo zikitapatapa zisiteremshwe daraja ya pili ya Bundesliga.Kwahivyo, zikawahonga wachezaji Fulani wa Braunschweig fedha.

Mahkama ya Ligi ikaihukumu Braunschweig:

“mchezaji Lothar Ulsass wa Braunschweig anafungiwa kucheza hadi mwisho wa msimu wa mwaka 71/72.Gharama za kesi zinamuangukia mchezaji mwenyewe dhamana ikibebeba klabu yake Eintracht Braunschweig.”Hivyo ndivyo ilivyokua.

Kutokana na kashfa hiyo, dimba zima la Ujerumani lilipepesuka.Idadi ya mashabiki ikaanza kupungua viwanjani na Eintrach Braunschweig ikaanza kukumbwa na misukossuko ya fedha.Wakuiokoa akatafutwa na akapatikana:Alikuwa Günter Mast.Mast alikuwa bepari la viwanda vya pombe na akisaka daima fikra za kupanua soko lake.

Matangazo ya biashara katika jazi zab timu yalipoanza ,Braunschweig ilikua ya kwanza kutembeza bidhaa katika mpambano wake na schalke 04 hapo 1973.1973,Eintracht Braunschweig ikajikuta inarudi katika Ligi ya kimkoa.Ilipopanda daraja ya kwanza 1974,Braunschweig ilifanya mapinduzi makubwa ilipomuajiri staid wa zamani wa Bayern munich alierejea kutoka Real Madrid,nchini Spain:Paul Breitner.Lakini, hata yeye hakuweza kuinusuru,kwani 1987 Eintracht Braunschweig ilizama daraja ya 3 na nje ya Bundesliga.