1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Elimu kwa wote: Washauri 4,000 washajiisha mafunzo ya chuo kikuu

Mohamed Dahman25 Juni 2012

Shirika la Watoto wa Wafanyakazi wa kawaida nchini Ujerumani linalojulikana kwenye mtandao kama Arbeiterkind.de linawashajiisha watu wasio na elimu ya chuo kikuu kujipatia elimu hiyo.

https://p.dw.com/p/15Hh7
Katja Urbatsch vwa m,radi wa "Initiative Arbeiterkind.de"
Katja Urbatsch vwa m,radi wa "Initiative Arbeiterkind.de"

Kinadharia haki ya kujipatia elimu ipo nchini Ujerumani lakini kwa vitendo inaonyesha kwamba watoto ambao wazazi wao hawana elimu ya vyuo vikuu mara chache sana huchaguwa kufanya mafunzo ya chuo kikuu. Shirika la Watoto wa wafanya kazi za kawaida linataka kubadilisha hali hiyo.

Katja Urbatsch ni mtu wa kwanza katika familia yake kufanikiwa kuingia chuo kikuu. Akikumbuka Katja mwenye umri wa miaka 32 anasema ''ilikuwa sio rahisi. Wazazi wangu walinishajiisha kuchukuwa mafunzo hayo lakini hawajaweza kunisaidia kikweli kweli''.

Hiyo ni kutokana na kwamba wazazi wake wenyewe hawakuwa na elimu ya chuo kikuu na kwa hiyo hawakuweza kumpatia mtoto wao huyo wa kike uzoefu wala maelekezo katika mafunzo yake. Hata hivyo Katja Urbatsh amefanikiwa katika mafunzo yake ya shahada ya pili ya masomo ya masuala ya Kimarekani, masuala ya umma na uchumi wa huduma ambapo hapo baadae alihitimu.

Anasema '' Ningelitaka watu wengine baada yangu mimi, suala la kuchukuwa mafunzo chuo kikuu liwe rahisi kwao.'' Yeye alihisi maisha aliyoyaita ya kichakani chuo kikuu yaani kuanzia uamuzi wa kuchaguwa masomo, kugharamia mafunzo yalikuwa magumu na yalihitaji nguvu.

Hapo mwaka 2008 aliweka habari zote muhimu kwenye tovuti ya mtandao kwa wale ambao hawazipati habari hizo nyumbani kama kitu cha kawaida, yaani kwa ajili ya watoto wa wafanyakazi wa kawaida. 

Mradi huo mdogo anaufanya bila ya malipo. Lakini siku moja baada ya kuzinduliwa kwa tovuti hiyo mtandaoni ni dhahiri kwamba juhudi hizo za Katja Urbatsch zinahitajika nchini Ujerumani. Anasema baada ya kuingia mtandaoni Jumapili, siku iliofuata Jumatatu alifanyiwa mahojiano na radio na yakafuata mahojiano mengi na maonyesho ya televisheni na maulizo bado yanaendelea bila ya kupunguwa ikiwa ni miaka minne badaa ya uzinduzi huo.

Washauri 4,000 wanashajiisha watu kujipatia elimu ya chuo kikuu

Utashi wa vyombo vya habari na zingatio la wananchi ni mambo yaliomshangaza Urtbasch. Kabla ya mpango wake huo ni dhahir kwamba kulikuwa hakuna mwamko katika jamii wa kuelewa kwamba inamaanisha nini kutoka kwenye familia ambapo hakuna mtu aliye na elimu ya chuo kikuu. Hata hivyo tayari takwimu kuhusu suala hilo zimekuwa zikijulikana kwa muda mrefu.

Vijana wa Kijerumani wakishiriki mafunzo ya ushajiishaji watu kujiunga na elimu ya chuo kikuu.
Vijana wa Kijerumani wakishiriki mafunzo ya ushajiishaji watu kujiunga na elimu ya chuo kikuu.Picha: Arbeiterkind

Takriban asilimia 70 ya watoto kutoka familia za wasomi wenye elimu ya chuo kikuu wanachaguwa kuingia chuo kikuu, wakati watoto kutoka familia za wafanyakazi wa kawaida wanaokwenda chuo kikuu ni asilimia 25. Katja Urbatsch anaona takwimu nyengine hususan muhimu ni kwamba ni nusu tu ya watoto wa wafanyakazi wa kawaida walifuzu kumaliza masomo yao ya darasa la kumi na sita wanaanza kwenda cho kikuu.

Urbatsch ambaye ni muasisi wa shirika la watoto wa wafanya kazi wa kawaida anataka kubadili hali hiyo. Anasema ''Mimi nataka kila mtu aweze kujifunza chuo kikuu bila ya kujali anatoka kwenye msingi wa familia gani katika jamii.'' Mbali na mtandao wao huo kuwa na mambo mengi zaidi katika kipindi cha miaka minne iliopita shirika hilo linaaishi kwa kutegemea juhudi za wenyeji kwa hivyo hivi sasa nchini kote Ujerumani kuna makundi manane yakiwa na washauri 4,000. Kwa mfano huwa wanashirikiana na shule na kuwaelekeza wanafunzi njia za kuweza kuingia chuo kikuu.

Fedha ni kikwazo

Sven Gramstadt ni mmoja wa washauri hao aliyeko katika kundi la Berlin.Yeye amesomea fundi uashi na kwanza hajaamini kama chuo kikuu ni ni kitu kinachofaa kwake. Anasema ''Mimi natokana na familia ya watu wanaofanya kazi za kawaida ambapo unaambiwa somea kitu cha maana, -jifunze kazi .''

Vijana wa Kijerumani wakishiriki mafunzo ya ushajiishaji watu kujiunga na elimu ya chuo kikuu.
Vijana wa Kijerumani wakishiriki mafunzo ya ushajiishaji watu kujiunga na elimu ya chuo kikuu.Picha: DW/Nadine Wojcik

Kwa njia tafauti ameweza kuingia chuo kikuu. Leo anachukuwa shahada yake katika somo la elimu ya watu wazima na anauelezea uzoefu wake kwa wanafunzi waliokuwa hawawezi kuamuwa wanataka kujifunza nini na waliokuwa hawajiamini ambao mwishowe hawapati kazi.

Kwa mfano huchaguwa masomo juu ya masuala ya ubinaadamu.Kwa mujibu wa Gramstadt anataka kuwashajiisha wanafunzi na anaona kwamba inasaidia hususan pale anapojuwa wanajihisi vipi,kwani yeye pia ametoka katika hali kama hiyo.

Mbali ya kuwatembelea huko mashuleni pia anaandaa muda wa kuzungumzia suala hilo kila mwezi mjini Berlin na mara nyingi mazungumzo yao hujikita kwenye suala la njia za kugharimia mafunzo hayo chuo kikuu. Nini wanapaswa kufanya iwapo wazazi wao hawawezi kuwasaidia kugharamia mafunzo hayo?

Kwa kweli suala la malipo nchini Ujerumani sio tatizo, kuna msaada wa serikali kwa kupatiwa mkopo bila ya riba pia kuna mashirika ambayo yanawasaidia wanafunzi wanaotoka kwenye familia zenye mapato hafifu. Mara nyingi kunakuwa hakuna moyo au maarifa ya kuomba fedha hizo.

Miaka minne baada ya kuunda shirika lake hilo Katja Ubertsch anaangalia kwa furaha mabadiliko ya kwanza katika jamii. Anasema ''Kuna mipango mingi mipya ya ufadhili wa mafunzo kwa kundi tunalolishughulikia. Tumetowa mchango mkubwa sana kuona mada hiyo inajadiliwa zadi kwenye vyombo vya habari na kwamba hivi wanasiasa wanafahamu vizuri zaidi hali ya watoto wa wazee wasiokuwa na elimu ya chuo kikuu. Urbatsh haoni kwamba kazi yake hiyo ni ya kiserikali.

Anasema kwa jinsi wanavyolishughulikia kundi lao kwa bidii kubwa hakuna taasisi ya serikali inayoweza kufanya hivyo na kwamba jambo hilo lazima litokane na mashirika ya kiraia ambayo yanaweza kulishughulikia jambo hilo vizuri zaidi.

Mwandishi: Wojcik,Nadine/Mohamed Dahman

Mhariri: Mohammed Abdul-Rahman