1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Erdogan aridhia mabadiliko ya katiba

10 Februari 2017

Rais wa Uturuki, Recep Tayyip Erdogan ameridhia muswada tata wa mabadiliko ya katiba ambao kwa kiasi kikubwa utamuongezea mamlaka rais huyo, huku kura ya maoni ikitarajiwa kupigwa ifikapo Aprili 16 mwaka huu. 

https://p.dw.com/p/2XM8O
Erdogan auf goldenem Thron
Picha: picture-alliance/AP Photo/H. Dridi

Waungaji mkono wa Erdogan wanauona mpango huo unaochukua nafasi ya bunge kwa kumpa mamlaka kamili Rais kuwa ni kama dhamana ya utulivu hasa katika kipindi hiki ambapo nchi hiyo inapitia mtikisiko mkubwa. Hata hivyo wapinzani wanahofu kuibuka kwa utawala wa kimabavu katika nchi hiyo ambayo imeshuhudia makumi kwa maelfu ya raia, kuanzia wanahabari hadi wanajeshi wakitiwa vizuizini tangu mapinduzi yaliyoshindwa mwezi Julai mwaka uliopita.

Taarifa fupi iliyotolewa kupitia tovuti ya rais imesema muswada huo utakaompa mamlaka Rais ya kutoa amri, kutangaza hali ya hatari, kuteua mawaziri na viongozi wa juu serikalini pamoja na kulivunja bunge umepelekwa kwenye ofisi ya Waziri mkuu kwa ajili ya kuchapishwa na kuwasilishwa kwa ajili ya kura ya maoni. 

Mapema mwezi huu, kwenye mkutano na waandishi wa habari pamoja na Kansela wa Ujerumani Angela Merkel alipofanya ziara nchini humo, Erdogan aliyatetea kwa nguvu mapendekezo ya mabadiliko hayo, ambayo bado yanakabiliwa na ukosoaji mkali kutoka kwa wapinzani wanaodai yatamuongezea mamlaka makubwa zaidi.

Türkei  Angela Merkel - Binali Yildirim
Rais Recep Tayyip Erdogan na Kansela wa Ujerumani Angela Merkel walipokuwa kwenye mkutano na waandishi wa habari nchini Uturuki Picha: picture alliance/ZUMAPRESS.com

Naibu waziri mkuu wa Uturuki, Numan Kurtulmus amewaambia wanahabari kwamba jukumu lililopo sasa ni kwa bodi ya uchaguzi ambayo itatakiwa kutangaza rasmi kwamba Aprili 16 ni siku maalumu kwa ajili ya kura ya maoni.

Kulingana na Erdogan, mabadiliko hayo yataepusha kurejea kwa muungano wa vyama ambao haukuwa na nguvu bungeni, lakini pia ni muhimu kwa wakati huu ambapo Uturuki inakabiliwa na vitisho vya kiusalama, hususan kutokana na mlolongo wa mashambulizi ya mabomu kutoka makundi ya Dola la Kiislamu, IS na wapiganaji wa Kikurdi pamoja na mapinduzi yaliyoshindwa.

Katika hatua nyingine, polisi nchini humo wamelazimika kutumia mabomu ya kutoa machozi kuwatawanya waandamanaji waliojaribu kuingia katika viunga vya chuo kikuu cha Ankara kupinga hatua ya serikali ya kuwafukuza wahadhiri 330. takriban waandamanaji 12 wanashikiliwa.

Wahadhiri hao ni miongoni mwa watumishi wa umma 4,500 waliotimuliwa siku ya Jumanne chini ya amri ya serikali ya hali ya hatari iliyotangzwa tangu mapinduzi yaliyofeli ya mwezi Julai mwaka uliopita.

Mwandishi: Lilian Mtono/AFPE
Mhariri: Josephat Charo