1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

F1: Vettel aibuka mshindi Canada

Bruce Amani
11 Juni 2018

Dereva wa timu ya Ferrari Sebastian Vettel alishinda mashindano ya Canada na kuchukua tena uongozi wa ubingwa wa dunia wa Formula One kutoka kwa dereva wa timu ya Mercedes Lewis Hamilton

https://p.dw.com/p/2zIug
Formel Eins, Kanada 2018: Sebastian Vettel
Picha: Reuters/C. Allegri

Ushindi huo ulikuwa wa 50 katika taaluma ya Mjerumani huyo na wake wa tatu msimu huu. Ulikuwa ushindi wa kwanza wa Ferrari nchini Canada tangu ule wa bingwa mara saba wa dunia Michael Schumacher katika mwaka wa 2004. Dereva wa Finland Valtteri Bottas alikuwa wa pili na timu ya Mercedes huku chipukizi Mholanzi Max Verstappen wa Red Bull akimaliza wa tatu. Hmilton alimaliza katika nafasi ya tano.

Nadal atwaa taji la French Open

Katika tennis Rafael Nadal anasisitiza kuwa hana hamu ya kuingia katika kinyang'anyiro na Roger Federer ili kumpiku mpinzani wake huyo mkuu ambaye ana mataji 20 makuu ya Grand slam.

Nadal alitwaa taji lake la 11 la mashindano ya French Open baada ya kupata ushindi wa seti za 6-4, 6-3, 6-2 dhidi ya Dominic Thiem hapo jana na kufikisha 17 mataji yake makuu.

Hiyo ina maana mataji matatu nyuma ya Federer ambaye anamzidi Nadal kwa miaka minne. Nadal mwenye umri wa miaka 32, anasema malengo ya aina hiyo hayampi mawazo yoyote.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/DPA
Mhariri:Mohammed Abdul-Rahman