1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

FIFA YATOA ORODHA YA TIMU BORA AFRIKA

Ramadhan Ali20 Septemba 2007

Nigeria inaongoza orodha mpya ikifuatwa na kamerun.Nafasi ya tatu inasimama Ivory Coast.

https://p.dw.com/p/CHb1

Avram Grant,aliekua mkurugenzi wa Chelsea,ndie kocha mpya baada ya kujiuzulu leo kwa Jose Mourinho.

FIFA leo imetoa orodha ya timu bora kabisa za Afrika na inaongozwa na Nigeria huku simba wa nyika Kamerun wakifuata nafasi ya pili.

Leo ni zamu ya kombe la UEFA na Bayern Munich inateremka uwanjani kucheza na Belenese ya Ureno.

Mashabiki wa Chelsea walistuka mapema leo kusikia kocha wao maarufu Jose Mourinho ameiachamkono klabu yao alieiongoza kutwaa mara mbili ubingwa wa premier League-Ligi ya Uingereza.

Taarifa zasema Mourinho amekorofishana na Abramovich,tajiri wa klabu ya Chelsea.Kocha mpya sasa atakuwa Avram Grant ,aliekuwa hadi sasa mkurugenzi.Grant –muisraeli ni kocha wa zamani wa timu ya taifa ya Israel na Abramovich aliinunua Chelsea , 2003.Mourinho alipinga kuteuliwa kwa grant hapo kabla kama mkurugenzi na mwishoe aliporidhia alionya asimuingile kazi zake.Chelsea ina miadi na Manchester United kwa duru ijayo ya Premier League.

Mabingwa wa Ujerumani Stuttgart,waliregeza kamba mbele ya Glasgow rangers katika kinyan’ganyiro cha champions League na mwishoe wakarudi nyumbani wamefungwa mabao 2:1.Ilikua lakini, Stuttgart ilioufumania kwanza mlango wa Rangers mnamo dakika ya 56 ya mchezo.Baadae Charlie Adam alisawazisha bao la Gomez na baada ya Hutton kupigwa mwereka na Fernando Meira katika eneo la adhabu,Darcheville aliusindikiza mkwaju wa penalty katika lango la Stuttgart kufanya mabao 2:1.

Meneja wa Stuttgart, Horst Held baadae alisema:

“Tumevunjika moyo kabisa.Haikupo haja ya kushindwa .Tumecheza uzuri na mabao 2 tuliotiwa yangeweza kuepukwa.”

Nae kocha wa Stuttgart Armin Veh,akikasirika alisema:

“Hii inaudhi sana.Halafu unabidi kukaa hapa na kueleza ilikuaje tumeshindwa kwa kuwa tu walinzi wetu mara 3 walillala .Inakera sana.”

Alisema kocha wa mabingwa wa Ujerumani Stuttgart.

Thierry Henry alitia bao lake la kwanza kwa FC Barcelona ya spain katika ushindi wao wa mabao 3:0 jana dhidi ya Lyon.

Christiano Ronaldo alilifumania lango la Sporting Lisbon,timu yake ya zamani na kuipatia Manchester United bao la ushindi.

FIFA imetoa orodha yake ya mwezi ya timu bora za Afrika: Nigeria inaongoza orodha hiyo ikifuatwa na samba wa nyika kamerun huko tembo wa Ivory Coast wakisimama nafasi ya 3.

Wakati zambia inasimama nafasi ya 11,Msumbiji imechupa hadi nafasi ya 16 nyuma ya Bafana Bafana-Afrika kusini.Uganda inasimama nafasi ya 24.Wakati Tanzania iko nafasi ya 26,Burundi imeangukia ngazi ya 29.Kenya iko nafasi ya 34.

Nusu-finali ya kombe la klabu bingwa barani Afrika inachezwa kesho kati ya Etoile du Sahel ya Tunisia na Al Hilal ya Sudan uwanjani Omduraman.Mabingwa al Ahly wana miadi jumapili na Al Ittihad ya Libya mjini Tripoli.