1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

G20:Ghasia mitaani joto la kisiasa kwa Merkel

8 Julai 2017

Mkutano wa Kilele wa G20 Hamburg, umegubikwa na maandamano ya mivutano ya kisiasa na jinsi mji huo unavyoweza kutumbukia katika  utawala wa ''makundi ya wahuni'' na kwa nini Kansela Angela Merkel aliuchagua mji huo.

https://p.dw.com/p/2gCO9
Deutschland, Hamburg, G 20
Picha: Reuters//H. Hanschke

Gazeti  la Kijerumani Bild linalotoka kila siku lilizungumzia kulaani kwake  machafuko yalioshuhudia wafuasi wa siasa kali za mrengo wa kushoto, wakiyawasha moto magari kadhaa, ku kutwaa ngawira madukani na  kupambana na  polisi wa kuzuwia fujo kwa mawe na chupa. Gazeti hilo katika toleo la leo liliandika; mtu anaweza kuyaita matukio ya Hamburg kama ni kushindwa kwa dola kuidhibiti hali ya mambo kwa saa 48 na  mkutano huo wa kilele kugeuka uwanja wa mapambano. Bila shaka  polisi walijitahidi kufanya kila wawezelo lakini mitaa ilidhibitiwa na  magenge ya wafanya  fujo.

Malalamiko na ukosoaji mkubwa  ulitolewa  pale polisi 20,000  katika mji huo alikozaliwa  Kansela Angela Merkel ulipoingia katika siku ya tatu ya vurugu kupinga mkutano huo wa G20, ambapo aliwakaribisha rais Donald Trump wa Marekani, Vladimir Putin wa Urusi na viongozi wengine wa dunia. Eneo la mkutano wao  ulifanyika kukiwa na ulinzi mkali, lilizungukwa  na  vizuizi vya barabarani vilivyowekwa na polisi, maduka yalioharibiwa na chupa na vigae vilivyozagaa kila mahali baada ya usiku wa vurumai, huku polisi waliokuwa na silaha wakiwatia nguvuni  wanaharakati , waliokuwa wakiwatupia mawe kutoka kwenye sakafu za majengo ya karibu. Kwa mtazamo wa mazingira yaliokuweko wa jarida la Bild , Ujumbe mahsusi kutoka Jiji la Hamburg  ulikuwa, Magenge ya wafanya fujo  yakitaka kutawala hutawala.

Polisi mmoja alimlaumu kansela Merkel na Meya wa Hamburg Olaf Scholz kwa kuruhusu hali hiyo ijitokeze, ambapo zaidi ya  polisi 200 na idadi isiyojulikana ya waandamanaji walijeruhiwa, na hasa wakalaumiwa kwa kuuchagua mji huo kuwa kituo cha mkutano wa kilele wa G20.

Kuchaguliwa kwa Hamburg

Deutschland, Hamburg, G20 Proteste
Polisi wakiwa tayari kukabiliana na waandamaji Hamburg.Picha: picture-alliance/N.Liponne

Kwa muda mrefu serikali ya Merkel imesisitiza kwamba kuuchagua mji huo  kuwa mahala  pa mkutano wa kilele wa G20, kumetokana na  mji huo kujitambulisha  kama  mji wa mchanganyiko wa watu wa tamaduni mbali mbali na" mlango wa kuelekea kwengineko duniani." Hoja nyengine ni kwamba kinyume na  miaka ya nyuma ambapo viongozi wamekuwa wakijifungia maeneo ya vijijini, kukutana kwao katika mji huo mkubwa kungeonesha kuwa hawajitengi na umma.

Kumefanyika takriban  mikutano ya hadhara 30 kupinga  mkusanyiko huo wa viongozi wa G20, kuanzia  maandamano ya amani na karamu za barabarani zikiandamana na muziki, hadi vizuizi barabarani na  upinzani kwa kutumia mashua baharini na machafuko  baada ya usiku kuingia.

Akitetea hatua zote hizo, Jana Schmeider kutoka muungano wa wanaopinga mkutano wa G20, amesema kuwa  mitaani ni sehemu ya waandamaji na sio mkutano wa kilele. Gazeti la  Spiegel katika matandao wake lilisema  bibi Merkel ambaye anakabiliwa na  uchaguzi mkuu Septemba 24, anapaswa kutambuwa kitakachokumbukwa zaidi ni picha za magari yanayowaka moto na wanaharakati wenye msimamo mkali na sio mkutano wa kilele wa G20.

Baada ya  siku mbili za mapambano makali na waandamanaji, polisi mjini Hamburg wameanza kazi ya kulisafisha eneo la karibu na mkutano huo wa G20.

Mwandishi: Mohammed Abdul-Rahman, afp,dpa

Mhariri: Daniel Gakuba