1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Gaddafi na harakati za kutaka mahusiano mapya na nchi za magharibi

Saumu Mwasimba25 Julai 2007

Rais Muammar Gaddafi wa Libya baada ya kutengwa kwa muda mrefu na nchi za Magharibi sasa aonekana kupania kujijenga kimataifa na kurudisha uhusiano na nchi hizo

https://p.dw.com/p/CHAV
Picha: AP

Rais wa Libya Muammar Gaddafi kiongozi pekee katika nchi za kiarabu aliyedumu kwa muda mrefu madarakani wakati mmoja alitengwa na nchi za magharibi kufuatia madai kwamba nchi yake ilihusika katika mashambulio ya kigaidi.Lakini sasa kiongozi huyo anaonekana amepania kuibuka tena na kuimarisha uhusiano wake na jumuiya ya kimataifa.

Wiki hii rais Muammar Gaddafi alifanikiwa kupata ahadi ya kurejesha uhusiano wa kawaida na Umoja wa Ulaya wenye wanachama 27 hii ikiwa ni sehemu ya makubaliano yaliyofikiwa juu ya kuwaachia huru matatibu sita wakibulgaria waliohukumiwa kunyongwa nchini Libya kwa kukutikana na hatia ya kuwaambukiza makusudi virusi vya HIV watoto wakilibya.

Makubaliano ambayo yalikuja baada ya miaka sita ya mazungumzo ya kina ya kidiplomasia.

Hali hiyo imefuatia tangazo la Marekani mwezi mei mwaka huu la kurudisha uhusiano wa kawaida na Libya pamoja na kuifuta nchi hiyo kwenye orodha ya nchi zinazounga mkono Ugaidi.

Libya baada tangazo lake la kihistoria la kuachana na utengenezaji wa silaha za maangamizi mnamo desemba mwaka 2003 rais Gaddafi aliapa kulirudisha taifa taifa lake katika kundi la watiifu duniani, kuwalipa ridhaa waathiriwa wa mashambulio ya mabomu yaliyodaiwa kudhaminiwa na utawala wake hii yote ni kwa ajili ya maendeleo ya Libya.

Hatua mpya za kutaka mjongeleano ambazo pia zimeibua hisia za nchi za magharibi za kutaka kuwa karibu na mali asili ya Libya zimeubadili msimamo mgumu wa rais Gaddafi aliokuwa nao katika kipindi cha miongo iliyopita.

Rais Gaddafi aliyezaliwa mwaka 1942 aligonga vichwa vya habari duniani mwaka 1969 aliponyakua madaraka kwa kuipindua serikali ya libya iliyokuwepo madarakani wakati huo ikiongozwa na mfalme Idriss.

Kutokana na kusukumwa na ndoto yake ya kutaka kuona Umoja wan chi za kiarabu na mtazamo wake wa kiislamu Gaddafi alijitenga na nchi za magharibi punde tu baada ya kunyakua madaraka akizishutumu kwa kuanzisha njama mpya dhidi ya waarabu.

Gaddafi akivutiwa zaidi na viongozi kama vile aliyekuwa rais wa Misri Gamal Abdel Nasser.

Gaddafi ni kiongozi ambaye anaegemea pande za Afrika na mataifa ya kiarabu amekuwa akipigania zaidi maendeleo ya bara la Afrika akimimina fedha katika kusaidia maendeleo kwenye eneo la Afrika kusini mwa jangwa la Sahara na kuunga mkono makundi mbali mbali ya kigaidi katika sehemu mbali mbali za dunia.

Kimataifa utawala wake uligubikwa na kushindwa kwa majaribio kadhaa ya kuungana na nchi zingine za kiarabu na kuunga mkono makundi ya itikadi kali.

Libya iliwagharimia kifedha au kuwatumia silaha makundi ya kipalestina yaliyona msimamo mkali na makundi mengine ya kutetea uhuru ikiwa ni pamoja na IRA Jeshi la jamhuri ya Ireland na waasi wa Moro nchini Uphilipino lakini kwake nchini Libya upinzani wowote haupewi nafasi kufurukuta.