1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

GAZA CITY : Hamas yadhibiti Gaza

14 Juni 2007
https://p.dw.com/p/CBrv

Wapiganaji wa kundi la Hamas takriban wamevitimuwa vikosi vyote vya kundi hasimu la Fatah kutoka Ukanda wa Gaza.

Watu zaidi ya 80 wameuwawa kufuatia mapigano makali ya siku kadhaa katika eneo hilo la Wapalestina.Milio ya bunduki za rashasha na mizinga imekuwa ikiendelea kusikika wakati wa usiku katika mji wa Gaza licha ya Rais Mahmoud Abbas kutoka kundi la Fatah na Waziri Mkuu Ismael Haniyeh wa kundi la Hamas kukubaliana kusitisha mapigano.

Rais Abbas wa Palestina amesema Gaza iko kwenye ukingo wa kusambaratika.

Rais Abbas amesema huo ni wendawazimu.Kile kinachotokea Gaza hivi sasa ni wendawazimu na kwamba kila mtu anahusika na hali hiyo kila mwenye kubeba silaha anahusika na hali hiyo haina budi kukomeshwa.

Rais huyo wa Pakestina leo anatazamiwa kutowa tangazo muhimu juu ya serikali ya umoja wa kitaifa inayoundwa na makundi hayo mawili ya Kipalestina ambayo imekumbwa na mfarakano na kuna hata uwezekano wa kundi la Fatah kujitowa kwenye serikali hiyo.

Wakati huo huo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki- moon amejibu ombi la Abbas la kutaka kuhusika kwa Umoja wa Mataifa ambapo amesema amejadili na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa uwezekano wa kuweka kikosi cha kimataifa kulinda amani huko Gaza.