1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Gaza yaendelea kuteketea,mashambulio ya ardhini ya Israeli yashika kasi

Saumu Mwasimba5 Januari 2009

Marekani yatetea mashambulio hayo ya Israel huku jumuiya ya kimataifa ikijitahidi kutafuta suluhu

https://p.dw.com/p/GRzv
Moshi unafuka baada ya mabomu kuangushwa na ndege za Israeli kwenye chuo kikuu cha kiislamu mjini Gaza kinachosimamiwa na Hamas.Picha: AP

Jeshi la nchi kavu la Israeli linaendelea kusonga mbele katika ukanda wa Gaza huku idadi ya wapalestina waliouwawa kufikia sasa kufuatia mashambulio ya wanajeshi ikiripotiwa kufikia zaidi ya watu 500.

Ujumbe wa Umoja wa ulaya umewasili katika eneo la mashariki ya kati ambapo wanatazamiwa hii leo kwenda Israeli na ukingo wa magharibi baada ya hapo jana kukutana na waziri wa mambo ya nje wa Misri.

Ujumbe huo unaongozwa na waziri wa mambo ya nje wa jamhuri ya Czech ambayo ni mwenyekiti wa sasa wa Umoja wa Ulaya akifuatana na waziri wa mambo ya nje wa Ufaransa Bernad Kouchner na Carl Bildt wa Sweden pamoja na kamishna wa masuala ya nje wa Umoja huo Benita Ferrero Waldner ambaye ametoa mwito kwa pande zote kukomesha mara moja mapigano na pia kuitaka Israeli isimamishe opresheni yake ya wanajeshi wa nchi kavu na angani.


Kwa upande mwingine katibu mkuu wa Umoja wa mataifa Ban Ki Moon ametoa masikitiko yake hapo jana baada ya baraza la usalama la Umoja wa mataifa kushindwa kufikia makubaliano katika kikao cha dharura juu ya kukomeswa kwa mashambulio ya Israel.

Marekani ilipinga taarifa ya pamoja ya baraza hilo ya kutaka kukomeshwa kwa matumizi ya nguvu ya Israeli na kundi la Hamas. Katibu mkuu amesema atakutana na wahusika wakuu kutoka nchi za kirabu pamoja na wanachama wa baraza hilo la usalama kutafuta suluhisho la haraka.

Rais Mahmoud Abbas na wmawaziri wa mambo ya nje kutoka nchi za kirabu watakuwa kwenye kikao hicho katika makao makuu ya Umoja wa mataifa mjini Newyork hii leo.Viongozi hao wanatarajia kuitolea mwito jumuiya ya kimataifa kuishinikiza Israeli kukomesha mashambulio ya Israeli dhidi ya Gaza.

Wakati huohuo kundi la Hamas linapanga kutuma ujumbe wake nchini Misri hii leo kwa ajili ya mazungumzo ya kwanza ya kidiplomasia tangu kuanza kwa oipresheni ya kijeshi ya Isreali dhidi ya Gaza.

Ziara hiyo ya Hamas imekuja wakati ambapo rais wa Ufaransa Nicolas Sarkozy pia anatarajiwa kufika Misri kwa lengo la kutia msukumo hatua za kidiplomasia na kufikiwa makubaliano ya amani.Aidha Tume ya Umoja wa Ulaya imeahidi kutoa euro millioni tatu zaidi kwa ajili ya msaada kwa watu wa Gaza.kamishna wa masuala ya misaada ya kiutu Loius Michel ametoa taarifa akisema kwamba hali ya kibinadamu kwa wakaazi milioni moja na nusu wa Gaza inazidi kuwa mbaya kila siku.

Pia ameitaka Israeli kuzingatia sheria za kimataifa na kuruhusu misaada iingie Gaza.